1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Genzebe Dibaba ana malengo makubwa

21 Machi 2016

Genzebe Dibaba analenga kupata mafanikio makubwa ya dadake katika michezo ya Olimpiki baada ya kufaulu kulitetea taji lake la mbio za mita 3,000 katika mashindano ya kimataifa ya riadha ya ukumbini mjini Portland, Oregon

https://p.dw.com/p/1IH3B
China Beijing 2015 IAAF Weltmeisterschaft Genzebe Dibaba
Picha: picture-alliance/dpa/S. Suki

Mwanariadha huyo wa mbio ndefu Muethiopia mwenye umri wa miaka 25 amezoea kuishi katika kivuli cha dadake mkubwa Tirunesh, mshindi mara tatu wa dhahabu katika michezo ya Olimpiki na bingwa mara tano wa dunia. Lakini sasa Dibaba amesema anaisaka dhahabu yake ya Olimpiki katika mashindano ya Rio mwezi Agosti baada ya ushindi wake wa jana. Na alipoulizwa vipi anavyofafanishwa na dadake, alisema mafanikio yake sio mengi kama ya Tirunesh, lakini ataendelea kufany abidii ili naye kufanikiwa hasa katika Olimpiki.

Ndoto ya msichana mkimbizi kuhusu Olimpiki

Msichana wa Kisyria Yusra Mardini amekabiliwa na vizuizi kama mkimbizi, kutoka nchi iliyoharibiwa na vita ambavyo watu wengi hawawezi hata kuanza kufikiria na sasa anataka kwenda katika Olimpiki ya Rio de Janeiro.

Muogoleaji huyo mwenye umri wa miaka 18 alitembea nchini Uturuki, akafunga safari ngumu na hatari ya baharini kwa kutumia boti hadi kisiwa cha Ugiriki cha Lesbos na taratibu akajikuta katika nchi za katikati ya Ulaya na dadake kabla ya kuwasili Berlin mwaka wa 2015. "Ni fursa ya kipekee maishani, fursa nzuri sana, nzuri kweli na hakuna atakayekuwa na fursa hii, hivyo nadhani nitafanya bidii kuhusu hilo.

Sasa ni sehemu ya kikundi cha wakimbizi 43 waliotambuliwa na kuchaguliwa na Kamati ya Kimataifa ya Olimpiki – IOC kuwa wanaolimpiki na wanapewa msaada katika harakati zao za kufuzu katika michezo hiyo. Mardini ambaye alifanya mchezo wa uogeleaji akiwa nyumbani Syria, alitafuta klabu ya kumsaidia kuyaona makali mara tu baada ya kuwasili Berlin. Aliipata fursa hiyo katika klabu ya mchezo wa uogeleaji ya Wasserfreunde Spandau "Tunafanya bidii sana kufuzu. Nadhani imekuwa ndoto yangu wakati nikiwa na umri wa miaka 12, au tangu nilipoanza kuogolea. Tunafanya kila tuwezalo ili kufuzu, kila mmoja ananisaidia, hivyo nadhani ntafuzu.

Wakimbizi watakaofuzu na kuunda timu ya kati ya wanamichezo 5 na 10 katika mashindano ya Rio watashiriki kama timu tifauti inayofahamika kama Wanamichezo Wakimbizi wa OlimpikI: Wataishi katika eneo moja na timu nyingine na watakuwa na haki sawa kama tu wanamichezo wengine 11,000.

Mwandish: Bruce Amani/AFP/AP/DPA/reuters
Mhariri: Saumu Yusuf