1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mueritrea ashinda dhahabu ya kwanza katika marathon

22 Agosti 2015

Wengi walitarajia kumwona mshikilizi wa rekodi ya dunia Mkenya Dennis Kimetto au mwenzake Wilson Kipsang au bingwa mtetezi wa dunia na Olimpiki Mganda Stephen Kiprotich akiibuka mshindi

https://p.dw.com/p/1GJrw
Ghebreslassie - Marathon,
Picha: Reuters

Lakini mambo hayakuwa hivyo, chipukizi kutoka Eritea Ghirmay Ghebreslassie aliwashangaza wengi kwa kunyakua dhahabu ya kwanza ya mashindano hayo.

Ghebreslassie mwenye umri wa miaka 19 alimzidi nguvu Tsepo Mathibelle wa Lesotho aliyeongoza mbio hizo kwa muda mrefu na kisha akampiku Muethiopia Yemane Tsegay na kushinda kwa muda wa saa mbili dakika 12 na sekunde 28.

Tsegay alinyakua fedha kwa kutumia muda wa saa mbili dakika 13 na sekunde nane huku medali ya shaba ikimwendelea Mganda Munyo Solomon Mutai aliyemaliza katika muda wa saa mbili dakika 13 na sekunde 30.

Ghebreslassie ndiye mwanaridha mwenye umri mdogo kabisa kuwahi kushinda dhahabu katika historia ya mashindano hayo.

Miamba wa Kenya walikabiliwa na wakati mgumu, huku Marek Korir akiwa mwanaridha aliyemaliza katika nafasi bora ya 22. Dennis Kimetto na Wilson Kipsang hawakumaliza mbio hizo katika mazingira ambayo yalikuwa magumu. Mganda Stephen Kiprotich alimaliza katika nafasi ya sita.

Lakini Ghebreslassie hakutatizwa na mazingira hayo akisema kuwa hali ya hewa ilikuwa nzuri sana, maana alikulia katika mazingira sawa na hayo.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/reuters
Mhariri: Mohamed Dahman