1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Guinea ya Ikweta na Zambia kutinga robo fainali

Sekione Kitojo28 Januari 2012

Guinea ya Ikweta na Zambia zina nafasi kubwa kuingia katika robo fainali ya kombe la mataifa ya Afrika wakati zitakapopambana katika mchezo wao wa mwisho wa kundi A , Jumapili.

https://p.dw.com/p/13sPC
Javier Balboa of Equatorial Guinea is surrounded by team mates after he scored the only goal of the match during the Africa Cup of Nations match between Equatorial Guinea and Libya in Bata, Equatorial Guinea, 21 January 2012. EPA/STR EDITORIAL USE ONLY
Javier Balboa wa Guinea ya Ikweta akishangiria bao.Picha: picture-alliance /dpa

Guinea ya Ikweta inahitaji point moja tu kuweza kuwa ya kwanza katika kundi A itakapokutana na Zambia leo jioni licha ya kuwa ni timu ambayo haikuwa na matumaini ya kufanya vizuri. Timu hizo zinakutana katika uwanja wenye uwezo wa kuingiza watazamaji 15,000 wa Nuevo Estadio de Malabo Jumapili ambapo kutakamilika moja kati ya mshangao mkubwa wa mafanikio katika duru ya kwanza ya historia ya miaka 55 ya fainali za kombe la mataifa ya Afrika mwaka huu.

Itaichukua timu hiyo inayoitwa kwa jina lake la utani la radi ya taifa katika robo fainali zitakazofanyika mwishoni mwa juma lijalo ikiwa nafasi ya juu inahakikisha mpambano wa mtoano dhidi ya Angola ama Sudan.

Licha ya kuwa sare itaihakikishia Zambia kusonga mbele katika kundi la timu nane zinazoingia katika duru ya mtoano , kikosi hicho cha Zambia , Chipolopolo, kinahitaji ushindi ili kuipiku Guinea ya Ikweta na kuepuka mpambano dhidi ya Cote D'Ivoire ambayo inaonekana kuwa huenda ikatoroka na taji la mwaka huu la kombe la Afrika.

Iwapo Zambia itapoteza mchezo kwa mara ya kwanza katika kinyang'anyiro hiki, Libya huenda ikachukua nafasi hiyo iwapo itafanikiwa kuishinda timu ambayo tayari imeshayaaga mashindano haya Senegal, simba wa teranga katika mchezo ambao utaanza kwa pamoja na ule wa Zambia na Guinea ya Ikweta mjini Bata.

Guinea ya Ikweta ina points sita, Zambia ikiwa na points nne, Libya moja na Senegal imeambulia patupu, na uhakika kuwa Simba hao wa Teranga wanafungasha virago na kurejea mjini Dakar vyovyote vile matokeo yatakavyokuwa.

A Senegalese soccer fan wearing face paint in her country's colors waits for her team to play Angola in a group D match in the African Cup of Nations in Tamale, Ghana, Sunday, Jan. 27, 2008. (AP Photo/Alastair Grant)
Shabiki wa timu ya taifa ya Senegal akishangaa matokeo ya timu yakePicha: AP

Wenyeji wenza wa mashindano haya wako katika nafasi ya 151 katika orodha ya timu bora za shirikisho la kandanda duniani FIFA na wamekuwa na matokeo mabaya sana katika wakati wa matayarisho katika michezo kadha ya kirafiki na kushindwa vibaya, ikiwa ni pamoja na kipigo cha mabao 4-1 dhidi ya Guinea Bisau, wanyonge wenzao , kabla ya kocha ambaye amefundisha timu mbali mbali kutoka Ufaransa Henri Michel kujiuzulu mara mbili kuifunza timu hiyo.

Aliombwa na kushawishwa kurejea mara baada ya kujiuzulu kwake mara ya kwanza , lakini kuondoka kwake chini ya mwezi mmoja kabla ya kuanza kwa mashindano haya kumeshuhudia kocha Mbrazil mwenye umri wa miaka 62 Gilson Paulo kushika hatamu za timu hiyo licha ya kutokuwa na uzoefu wa kuifunza timu ya taifa.

Ilionekana kuwa maafa yanaelekea kuikumba timu hiyo ya Guinea ya Ikweta , lakini mchezaji wa katikati , nahodha wa muda na msemaji ambaye si rasmi wa timu hiyo Juvenal Edjogo alifurahi kuona Michel anafikia mwisho wa kuifunza timu hiyo na sera zake za kuchagua wachezaji ambao wengi wao wanachezea nchini humo.

Kikosi cha kwanza katika ushindi dhidi ya Libya na Senegal kilijumuisha wachezaji sita waliozaliwa Hispania ambao walikubalika kuchezea timu hiyo kwa kuwa mzazi mmoja ama babu anatokea katika nchi ndogo iliyoko katika bara la Afrika na pia katika visiwa vidogo vya nchi hiyo ya Afrika ya magharibi ambayo ina utajiri mkubwa wa mafuta na gesi.