1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hali ni tete nchini Yemen

26 Septemba 2011

Upande wa upinzani nchini Yemen umekula kiapo dhidi ya rais Ali Abdallah Saleh wanaedai hatekelezi ahadi anazotoa na hasemi lini atang'oka madarakani.

https://p.dw.com/p/12glN
Rais Ali Abdallah SalehPicha: dapd

Akihutubia taifa kwa njia ya televisheni jana usiku,rais Ali Abdallah Saleh alisema yuko tayari kukabidhi madaraka kwa amani baada ya uchaguzi na akaahidi kuanzisha kipindi cha mpito kama ilivyopendekezwa na baraza la ushirikiano la nchi za Ghuba.

Lakini Ali Abdallah Saleh anaeiongoza Yemen tangu miaka 33 iliyopita hakutoa pendekezo lolote thabiti na wapinzani wake wanakosoa kile wanachokiona kuwa ni "maneno matupu tu."

"Hotuba yake imelenga kuzidisha vurugu na sio kuufumbua mzozo" amesema Abdallah Magany,professor wa baiolojia aliyepiga kambi katika "Uwanja wa mageuzi" uwanja mkubwa wa mjini Sanaa unaodhibitiwa na wapenda mageuzi .

Mwenzake,Dr.Mohammed Al Qubati anatoa mwito akisema:

"Tunazitolea mwito pande zote muhimu,mashirika ya misaada ya kiutu,Umoja wa mataifa,Umoja wa Ulaya,mabalozi wote wa nchi za nje walioko katika nchi yetu watekeleze jukumu lao la kiutu kukomesha mauwaji.Walioko nyuma ya mauwaji haya wamepoteza hadhi na uhalali wao."

Jemen Sanaa Protest Demonstration Saleh Beerdigung
Waandamanaji wabeba jeneza kwaajili ya mazishi ya rais Ali Abdallah SalehPicha: dapd

Hali ilikuwa tulivu kidogo hii leo katika eneo la kati la mji mkuu Sanaa baada ya machafuko ya wiki nzima kati ya waandamanaji na vikosi vya usalama-yaliyoangamiza maisha ya zaidi ya watu mia moja.

"Saleh anabidi atie saini haraka mkataba wa kung'oka madarakani la sivyo mapigano yataendelea na sisi tutasalia upande wa waandamanaji," amesema Rashad Ali Mohsen ambae ni mwanajeshi.

Jemen Universität in Sanaa Unruhen
Chuo kikuu cha Sanaa kimegeuka kitovu cha maandamanoPicha: DW

Katika hotuba yake ya jana,ya kwanza tangu aliporejea nyumbani kutoka Saudi Arabia ambako alipata matibabu baada ya kujeruhiwa vibaya sana ,kasri lake liliposhambuliwa kwa mabomu mwezi June mwaka huu,rais Ali Abdallah Saleh alisema anaukubali mpango wa kukabidhi madaraka ulioandaliwa na baraza la Ushirikiano la nchi za Ghuba.Lakini mara tatu alikuwa nusra atie saini mpango huo kabla ya kubadilisha fikra dakika ya mwisho.

Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Reuters/Afp

Mhariri:Mohammed Abdul-Rahman