1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hali ya baadaye ya Opel inashikiliwa na uzi.

Sekione Kitojo28 Mei 2009

Uhai wa Opel unashikiliwa na uzi licha ya mkutano uliofanyika katika ofisi ya Kansela siku ya Alhamis. Kwa kuwa hakuna suluhisho lililopatikana.

https://p.dw.com/p/Hzai
Bango la kampuni ya Opel mjini Rüsselheim nchini Ujerumani.Picha: picture alliance / dpa

Pamoja na kikao cha juu kilichofanyika katika ofisi ya kansela, bado lakini hali ya baadaye ya kampuni la kuunda magari la Opel inapitia katika uzi mwembamba. Serikali ya Ujerumani , makampuni yanayotarajia kuinunua Opel ,wawakilishi wa kampuni mama ya General Motors pamoja na serikali ya Marekani pamoja na mawaziri wakuu kutoka majimbo nchini Ujerumani ambako kuna viwanda vya Opel , hawakuweza kupata suluhisho, la kuiokoa Opel kutoka katika hali ya kufilisika kwa kampuni mama la General Motors.

Wafanyakazi 26,000 wanaofanyakazi katika kampuni la kuunda magari la Opel nchini Ujerumani, pamoja na wafanyakazi wa viwanda vingine vya General Motors katika bara la Ulaya , wanawasiwasi na ajira zao. Ni kwa kuwa mkutano uliofanyika katika ofisi ya kansela, usiku wa Jumatano kuamkia Alhamis haukupata jibu lolote, hivi sasa ni wawekezaji wawili tu wanaoshiriki katika majadiliano. Kampuni la uwekezaji la Marekani Rippelwood limeondolewa katika orodha ya wanaoomba kununua kampuni ya Opel. Kwa upande wa wawekezaji hivi sasa kuna kampuni la Canada la utengenezaji wa vipuri vya magari , Magna , na kampuni la kuunda magari la Italia , FIAT.

Ndio sababu kwamba Opel kwa hivi sasa haiko katika hatari kubwa ya kutumbukia katika mporomoko wa kampuni mama ya General Motors inayokaribia kufilisika.

Badala yake kuna baadhi ya mahitaji yanayotakiwa kutekelezwa, kama kurejesha hati miliki ya Opel iliyoko Marekani hadi Ujerumani.

Pia kuna suala la mtiririko wa fedha uliokatika kati ya Opel na General Motors na viwanda vingine vya magari katika bara la Ulaya vinataka pia kuinunua Opel.

Lakini hii haitoshi. Ni lazima Opel ijitenge na kampuni yake mama ya Marekani.

Ni muhimu , kwamba Opel na viwanda vingene vya magari katika bara la Ulaya visiingie katika utaratibu mmoja wa kufilisiwa kampuni la General Motors nchini Marekani. Kama mkakati wa suluhisho la kisheria ambalo serikali ya Ujerumani imeliona, Opel inabidi kuchukuliwa na mwekezaji wa kuaminika, ambaye ataiongoza kampuni hiyo hadi pale mwekezaji kamili atakapopatikana.

Ni wazi kuwa suluhisho hili la kuwa na fedha za kuanzia ni muhimu. Kwa kuwa kuna Euro bilioni 1.5 zilizotengwa kutoka serikali pamoja na serikali za majimbo.

Mshangao ulikuwa mkubwa katika ofisi ya kansela , wakati General Motors, ghafla ilipandisha ombi la msaada na kufikia Euro bilioni 1.8.

Pamoja na hayo kwa mshangao mkubwa , serikali ya Marekani , ambayo wakati huo huo ni mfadhili mkubwa wa kampuni la General Motors, haukutuma mwakilishwa wa ngazi ya juu mwenye mamlaka ya kutoa uamuzi.

Kuna dhana kwamba General Motors na serikali ya Marekani hazina shauku ya kujua hali ya baadaye ya kampuni la Opel. Hii ni masikitiko makubwa, kwa kuwa mwishowe hali ya baadaye ya Opel itaamuliwa huko Detroit na mjini Washington. Serikali ya Ujerumani inasaidia sana kuweza kumpata muwekezaji, ambaye atakuwa tayari na fedha za kugharamia pamoja na kuwa na uwezo wa kukopa mabilioni kadha ya Euro kutoka katika mabenki.

Kwa hiyo General Motors itabidi kuamua, ni nani hapo baadaye kwa Opel na makampuni yake mengine ya kuunda magari katika bara la Ulaya itakuwa na usemi wa mwisho. Kampuni la General Motors linapumua kwa msaada wa wizara ya fedha ya Marekani, pia lina mambo muhimu ya kuzungumza na serikali ya Marekani mjini Washington.


Mwandishi Zawadzky,Karl/ Sekione Kitojo

Mhariri Abdul-Rahman.


►◄