1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hamid Karzai ziarani Berlin

Bernd Grässler / Maja Dreyer19 Machi 2007

Rais Hamid Karzai wa Afghanistan ambaye yuko ziarani nchini Ujerumani, ameomba msaada wa kujenga upya nchi yake na kuhakikisha amani iendelee. Leo asubuhi rais Karzai alikaribishwa na Kansela wa Ujerumani, Bibi Angela Merkel.

https://p.dw.com/p/CHHx
Hamid Karsai na Angela Merkel
Hamid Karsai na Angela MerkelPicha: AP

Kwenye mkutano wao walizungumzia masuala nyeti kama vile: kushambuliwa jeshi la Ujerumani nchini Afghanistan, kupelekwa kwa ndege za kivita aina ya Tornado na vitisho vya magaidi.

Misaada ya Ujerumani kwa Afghanistan inazingatia hasa kazi za kujenga upya nchi hii. Haya aliyasema Kansela Angela Merkel baada ya mkutano wake na rais Hamid Karzai wa Afghanistan: “Lazima kufanya bidii katika miradi ya kujenga miundo mbinu. Mimi naona upatikanaji wa umeme ni muhimu sana. Kutokana na uzoefu tulio nao tuna hakika kuwa mkakati wetu wa kushughulikia sekta mbali mbali unafaa, yaani sio jeshi peke yake, au msaada wa maendeleo mbayo iunaweza kusuluhisha hali hii, bali ni yote haya mawili kwa pamoja.”

Rais wa Afghanistan alisifu msaada unaotolewa na Ujerumani kwa ujumla, akisisitiza juu ya uamuzi uliochukuliwa hivi karibuni wa kutuma ndege za kivita za ukaguzi wa anga nchini Afghanistan. Alisema ndege hizo hazina umuhimu wa kijeshi tu bali pia kuwapa Wafghanistani hisia za usalama.

Akiuulizwa ana maombi gani kwa Ujerumani, Karzai alisema hivi:´“Yale ambayo Ujerumani inayafanya nchini Afghanistan ni mazuri sana, na jamii ya Afghanistan inatoa shukrani zake. Kuongeza juhudi zake nchini Afghanistan ni juu ya Wajerumani wenyewe. Sisi Waafghanistani tutaukaribisha uamuzi wowote Wajerumani watakaouchukua kuhusiana na usalama na kujenga upya Afghanistan.”

Kabla ya hapo, rais Karzai aliitaka serikali ya Ujerumani ifanye bidii kubwa katika kuelimisha na kutoa vifaa kwa maafisa wa usalama wa Afghanistan. Alisema kufanya hivyo kutapunguza gharama za jeshi la kimataifa katika siku za usoni alisema Karzai.

Yaliyozungumziwa ni pamoja na utekaji nyara wa Wajerumani wawili nchini Iraq. Watekaji nyara walidai Ujerumani itoe jeshi lake kutoka Afghanistan. Kwa sasa kuna wanajeshi 3150 wa Ujerumani nchini Afghanistan. Kansela Merkel alisema kamati ya dharura ya serikali inajitahidi sana, lakini serikali yake haitakubali kutozwa hongo. Alisema: “Ukweli huu si rahisi, lakini hivyo ndivyo serikali ya Ujerumani itakavyoendelea. Na mimi ninaamini njia hii inawahusu wote wanaojitolea kuijenga upya Afghanistan.”

Rais Karzai anamuunga mkono Bibi Merkel akisema kwa kukubali masharti ya watekaji nyara kutazidisha matumizi ya nguvu na ugaidi nchini humo.