1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hatima ya Uingereza katika Ulaya kujulikana Alhamisi

22 Juni 2016

Kampeni za lala salama kuunga mkono hatua ya Uingereza kubakia katika Umoja wa Ulaya au la, zinaendelea nchini humo, kabla ya kufanyika kwa kura ya maoni Alhamisi.

https://p.dw.com/p/1JBPU
Picha: DW/C. Ricking

Meya wa zamani wa jiji la London, Boris Johnson, mtu muhimu katika kampeni ya kutaka Uingereza ijiondoe kwenye Umoja wa Ulaya, amezunguka kwa mara ya mwisho kwenye mji huo akiwashawishi wapiga kura wakubali kujiondoa kwenye umoja huo.

Akizungumza kwenye soko kubwa na maarufu la kuuza samaki la Billingsgate, Johnson amesema Umoja wa Ulaya umekuwa ukifanya maamuzi kwa ajili ya Uingereza ikiwemo kuhusu jinsi ya kudhibiti uvuvi.

''Asilimia 60 ya sheria zinatoka Brussels, sekta ya uvuvi inadhibitiwa na Brussels. Kuna halmashauri ya Umoja wa Ulaya ambayo inakaa kwa niaba yetu na kuamua jinsi samaki wetu wa Uingereza watakavyogawanywa. Hivyo kuchukua tena udhibiti nadhani itakuwa hatua kubwa na muhimu kwa demokrasia kwenye nchi yetu na Ulaya,'' amesema Johnson.

Boris Johnson
Boris JohnsonPicha: Getty Images/B. Pruchnie

Johnson amesisitiza kuwa umefika muda wa kuzungumzia demokrasia na mamilioni ya watu kuzunguka Ulaya wanakubaliana nao na kwamba ni wakati wa kujiondoa kutoka kwenye mfumo wa Umoja wa Ulaya ambao umeshindwa na usiofanya kazi zake vizuri.

Kwa upande wake Waziri Mkuu wa Uingereza, David Cameron anayeunga mkono nchi hiyo kubakia kwenye Umoja wa Ulaya, ameelezea mtazamo wake kuhusu mustakabali wa Uingereza kama itaendelea kubakia kwenye umoja huo wenye nchi wanachama 28.

Uingereza inanufaika Umoja wa Ulaya

Akizungumza leo na Shirika la Utangazaji la Uingereza-BBC, Cameron amesema nchi hiyo inanufaika kutokana na kuwa mwanachama wa Umoja wa Ulaya na amekanusha nadharia kwamba nchi hiyo itapotea iwapo itaendelea kubakia kwenye umoja huo.

Wakati huo huo, viongozi mbalimbali duniani wameitolea wito Uingereza kubakia kwenye Umoja wa Ulaya, akiwemo Rais wa Marekani Barack Obama, Kansela wa Ujerumani, Angela Merkel, Rais wa China, Xi Jinping, Jumuiya ya Kujihami ya NATO pamoja na nchi washirika za Jumuiya ya Madola.

David Cameron
David CameronPicha: picture-alliance/Daily Mail/PA Wire/K. Davies

Merkel amesema ana matumaini kwamba wapiga kura watapendelea kubakia kwenye Umoja wa Ulaya, lakini suala hilo ni juu ya Waingereza wenyewe kuamua.

Rais wa Ufaransa, Francois Hollande ameonya iwapo Waingereza watapiga kura kujiondoa kwenye Umoja wa Ulaya, utakuwa uamuzi usioweza kubadilika na ambao unaweza kuwa na hatari kubwa kwa Uingereza kuwepo katika soko la pamoja na uchumi wa Ulaya kwa ujumla.

Naye Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki, Mevlut Cavusoglu amesema sio sahihi hadhi ya Uturuki kama mwanachama wa Umoja wa Ulaya, kutumika kama hoja katika kampeni ya Uingereza kujiondoa kwenye umoja huo au la. Amesema Uturuki kamwe haijawahi kuwa mzigo katika umoja huo na ameongeza kwamba Uturuki itapendelea Uingereza ibakie katika umoja huo.

Mwandishi: Grace Patricia Kabogo/RTR, DPA,AP,AFP
Mhariri: Mohammed Khelef