1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Heiligendamm. Mazungumzo tete yaanza rasmi leo.

7 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBu2

Rais wa Marekani George W. Bush anatarajiwa kueleza wasi wasi wake juu ya uhuru wa kidemokrasia nchini Russia kwa rais Vladimir Putin wakati mkutano wa G8 utakapoingia katika siku yake ya pili mjini Heiligendamm nchini Ujerumani.

Putin hapo kabla amemuonya rais wa Marekani kutoingilia mambo ya ndani ya Russia.

Suala la mabadiliko ya hali ya hewa duniani liko katika ajenda ya leo katika mkutano huo wa G8, lakini Bush amekanusha kuwa kutakuwa na makubaliano katika mkutano huo ambayo yanahitaji upunguzaji mkubwa wa gesi zinazochafua mazingira.

Hata hivyo amedokeza kuwa anania ya kulishughulikia suala hili la mabadiliko ya hali ya hewa.

ushKansela wa Ujerumani Angela Merkel anatoa wito wa kuweka viwango maalum ambavyo vitahusisha umoja wa mataifa katika kuweka malengo ya kufikiwa ya utoaji wa gesi hizo.

Wakati huo huo gazeti la Financial Times linaripoti kuwa viongozi wa kundi la mataifa ya G8 wanaonekana kuwa watavunja ahadi ya kutoa msaada kwa waathirika wa ugonjwa wa ukimwi.

Gazeti hilo linazungumzia ripoti inayotoa wazo kuwa kundi la G8 linalengo la kutoa tiba ya dawa za kurefusha maisha kwa wahanga zaidi ya milioni tano katika muda wa miaka michache ijayo, na sio watu milioni 10 ifikapo mwaka 2010 kama ilivyoahidiwa katika mkutano kama huo mjini Gleneagles nchini Scotland miaka miwili iliyopita.