1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Horst Köhler aagwa rasmi.

Halima Nyanza16 Juni 2010

Viongozi mbalimbali wa serikali ya Ujerumani jana walihudhuria hafla ya kuagwa rasmi kwa Rais Hörst Köhler, aliyetangaza kujiuzulu ghafla mwishoni mwa mwezi ulipita, hali iliyosababisha mshangao mkubwa.

https://p.dw.com/p/Ns1i
Rais wa Ujerumani aliyejiuzulu hiki karibuni Horst Köhler (wa pili kushoto) wakati alipoagwa rasmi jana. kulia kwake ni Rais wa muda wa Ujerumani Jens Böhrnsen, na kushoto kwake ni Waziri wa Ulinzi wa Ujerumani Karl-Theodor zu Guttenberg.Picha: picture-alliance/dpa

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel na mumewe ambao ni nadra kufuatana pamoja hadharani walihudhuria pia hafla hiyo akiwemo pia Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje Guido Westerwelle, na Waziri wa Ulinzi Karl Theodor zu Gutenberg.

Kuhudhuria kwa viongozi hao kumeonesha pia kama ni kuondoa tetesi za kuwepo tofauti baina yao na Rais Köhler.

Horst köhler mwenye umri wa miaka 67, hakutoa sababu zozote juu ya uamuzi wake wa kujiuzulu wakati akiwashukuru wafanyakazi takriban 120 waliokusanyika katika makaazi ya rais mjini Berlin kutokana na kazi yake nzuri aliyoifanya madarakani katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.

Katika sherehe ya kumuaga Horst köhler aliwaalika ndugu na marafiki wa karibu wapatao 200 katika sherehe ya kumuaga jana jioni, huku kikosi cha jeshi la Ujerumani kiking´arisha silaha na viatu vyao kujiandaa na gwaride hilo la heshima kumuaga lililohudhuriwa na Kansela Merkel na mawaziri kutoka wizara nyeti.

Na miongoni mwa nyimbo alizopenda kupigiwa Rais Köhler wakati wa kumuaga ni wimbo wa miondoko ya jazz wa St. Louis Blues uliopigwa na bendi ya jeshi, Brass band.

Rais Köhler alilazimika kutangaza kujiuzulu Mei 31, kufuatia kukosolewa kutokana na mahojiano aliyoyafanya radioni, ambapo alisema kuwa jeshi la Ujerumani linabidi kutetea maslahi ya kitaifa ya Ujerumani ikiwemo biashara.

Kauli hiyo ilipingwa na watu wanaopinga vita pamoja na wanasiasa wa mrengo wa shoto.

Mojawapo ya kazi za Rais wa Ujerumani ni kulienzi jeshi.

Rais Köhler ambaye alijiuzulu, alisema kwamba ukosoaji dhidi yake ulivuka mipaka na kuvunja heshima ya wadhifa wake.

Rais Köhler alihalalisha hatua ya kujiuzulu ingawa si mbele ya vyombo vya habari na alisema kuwa hapakuonesha heshima ya wadhifa wake wa Urais, ukweli lazima uwe na sehemu yake katika siasa.

Watafiti wa mambo wanasema kuwa Hörst Kohler alifadhaishwa kwamba serikali haikujibu tuhuma hizo zilizotolewa dhidi yake.

Toka kujiuzulu kwake nafasi yake kwa muda imechukuliwa na spika wa bunge la Ujerumani, Jens Boehrnsen.

Na kwamba tayari vyama mbalimbali vya siasa vimetangaza majina ya mtu wao atakayechukua nafasi hiyo ya Urais huku muungano wa vyama vinavyoongozwa na Kansela Merkel vikimteua waziri mkuu wa jimbo la Lower Saxony Christian Wulff kuwa mgombea wa kiti cha urais.

Vyama vya upinzani vya SPD na kile cha kijani vimemchagua mwanaharakati za kiraia wa iliyokuwa Ujerumani mashariki Joachim Gauck kuwa mgombea wake.

Hata hivyo mgombea kutoka katika muungano wa bibi Merkel, Christian Wulff anaelekea kushinda nafasi hiyo, kutokana na muungano huo kuwa na wabunge wengi katika baraza la wawakilishi ambalo ndilo linalomchagua rais.

Mwandishi: Halima Nyanza(dpa)

Mhariri: Josephat Charo