1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hujuma zaendelea Gaza

Oumilkher Hamidou30 Desemba 2008

Israel yasema haiko tayari kuweka chini silaha kwa sasa

https://p.dw.com/p/GPAX
Majeruhi wa mashambulio ya IsraelPicha: AP



Israel imelikataa shauri la kuweka chini silaha huko Gaza,na kusema jeshi lake liko tayari kuendelea na na opereshini zake kwa muda mrefu dhidi ya Hamas.Hujuma za madege ya kivita ya Israel zinaendelea kwa siku ya nne hii leo.


 Vifaru na wanajeshi wamekusanywa katika eneo lote la mpakani,hali inayoashiria uwezekano wa kuingilia kati wakati wowote ule kutoka sasa,vikosi vya nchi kavu vya Israel katika Gaza.


Wakati huo huo hujuma za angani dhidi ya vituo vya Hamas zinaendelea ,wapalastina 12 wameuwawa,wakiwemo watoto wawili wadogo wa kike katika mji wa Beit Hanoun,kaskazini mwa Gaza.


Majengo matano ya wizara za utawala wa ndani na jengo la chuo kikuu cha Gaza yamebomolewa,sawa na kituo cha michezo na viwanja vya mazowezi.

Makombora kadhaa yamepiga katika nyumba ya kiongozi mmoja wa Hamas ambae hajakuwepo nyumbani kwake.


Hujuma hizi za leo zimetokea muda mfupi baada ya makombora ya wanamgambo wa Hamas kufyetuliwa na kuwauwa wayahudi wawili, mwanajeshi mmoja na raia mmoja huko Ashdod.


Wiki sita kabla ya uchaguzi wa bunge ambao kwa mujibu wa utafiti wa maoni ya umma,utakipatia ushindi chama cha mrengo wa kulia cha Likoud,serikali inashikilia lengo la hujuma hizi ni kukomesha mashambulio ya Hamas dhidi ya Israel.


"Hakuna wakati wa kuweka chini silaha" amesema waziri wa mambo ya ndani Meir Sheetrit kupitia Radio Israel na kuongeza tunanukuu:Jeshi la Israel halibidi kusitisha opereshini hii kabla ya kuvunja azma ya Hamas ya kuendelea kuishambulia Israel."Mwisho wa kumnukuu waziri wa mambo ya ndani wa Israel.


Wakati huo huo Israel imesema itaruhusu malori yaliyosheheni misaada ya kiutu na magari kama 20 hivi yaingie Gaza hii leo.


Waandishi vitabu watatu mashuhuri wa Israel wametoa mwito silaha ziwekwe chini haraka. Amoz Oz anasema


"Nnaamini Hamas ndio wanaobeba dhamana ya yanayotokea Gaza hivi sasa.Wanabeba dhamana moja kwa moja..Lakini linapohusika suala la Israel,nadhani wakati umefika wa kufikiria kuweka chini silaha.Tunatafuta nini Gaza.Kwa maoni yangu,hatufuati lengo jengine isipokua hatari ya kuzama katika janga la Gaza ambalo linaweza kuwa kubwa zaidi kupita lile la Libnan."


Mwenzake David Grossman ameliambia gazeti la Haaretz,"ingekua bora kama Israel itazuwia wenyewe na moja kwa moja hujuma hizo mnamo muda wa saa 48 zijazo,ili kama alivyosema," kuepukana na kuzidi idadi ya wahanga na uharibifu."


Kwa mujibu watarakimu zilizochapishwa Gaza,hujuma zilizoanza tangu jumamosi iliyopita zimegharimu maisha ya watu wasiopungua 360 na karibu 1700 kujeruhiwa.Nchini Israel waliouwawa kutokana na makombora ya Hamas ni watu wanne.