1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Iran imejibu mapendekezo ya nchi za magharibi juu ya kuumaliza mvutano kuhusu shughuli zake za kinuklia

Saumu Mwasimba4 Julai 2008

Je Kweli Iran itasimamisha urutubishaji wa Uranium? Wadadisi hawafikirii litawezekana

https://p.dw.com/p/EWYe
''Nchi za magharibi zinaitaka Iran ikifunge kinu chake hiki kikuu cha kurutubisha madini ya Uranium''Picha: AP

Majibu ya Iran hayajafafanuliwa lakini yamekabidhiwa mkuu wa sera za nje wa Umoja wa Ulaya Javier Solana mjini Brussels Ubelgiji hii leo. hayo ni kwa mujibu wa televisheni ya taifa ya Iran.Aidha Solana amefanya mazungumzo kwa njia ya simu na mjumbe wa Iran anayehusika na suala la Nuklia Saeed Jalili na kuyataja mazungumzo hayo kuwa yenye kutoa matumaini katika kuumaliza mvutano juu ya mpango wa kinuklia wa Iran.

Televisheni ya taifa ya Iran imetangaza kwamba nchi hiyo imeshatoa majibu yake juu ya mapendekezo ya kimataifa ya vivutio vya kiuchumi kibiashra na vinginevyo ikiwa nchi hiyo itakongoa kinu chake kikuu cha kinuklia.Ripoti hiyo lakini haijaeleza nini hasa kimetajwa katika barua hiyo ya majibu ya Iran.Televisheni ya taifa ya Iran badala yake inasema mjumbe wa Iran katika suala hilo la nuklia Saedda Jalili amemwambia mkuu wa sera za nje wa umoja wa Ulaya Javier Solana kwa njia ya simu kwamba Iran imeshawasilisha majibu yake kuhusu mapendekezo yaliyotolewa na nchi sita za magharibi zinazohusika zaidi katika mzozo huo.Kwa mujibu wa kituo hicho barua ya Iran imeandikiwa Solana kwa niaba ya nchi hizo sita,Uingereza,Ufaransa,Urussi,China Marekani na Ujerumani imetiwa saini na waziri wake wa mambo ya nje Manoucher Mottaki na kuwasilishwa na balozi wake mjini Brussels. Aidha ripoti za kituo hicho cha televisheni cha Iran zinasema Solana na Jalili wamekubaliana katika mazungumzo yao kuandaa mkutano hivi karibuni utkaofuatiliwa na mikutano mingine kadhaa katika kipindi cha nusu ya mwezi huu wa july.Kwa upande mwingine msemaji wa Solana Cristina Gallach amesema mpatanishi wa Iran katika mazungumzo ya Nuklia Saeed Jalili ametangaza kwamba atatuma majibu hivi karibuni kuhusiana mapendekezo ya kimataifa ya vivutio vinavyolengwa kuishawishi Iran kukomesha shughuli zake za kurutubisha madini ya Uranium.Cristina amesisitiza kwamba hata ikiwa watapata majibu rasmi ya Iran kuhusiana na suala hilo watahitaji muda fulani kutathmini jibu la Iran.Itakumbukwa kwamba nchi za magharibi mwezi ulopita zilitoa vishasiwishi vikiwemo vya kiuchumi na kisiasa lakini pendekezeko kubwa zaidi ilikuwa kuitaka Iran ikomeshe shughuli zake za kinuklia lakini katika jibu la Iran hii leo haijawekwa wazi ikiwa nchi hiyo imekubaliano na takwa hilo la nchi za magharibi ingawa wachambuzi wa mambo wanatilia shaka ikiwa Iran kweli itafikia makubaliano kuhusiana na suala hilo.Wadadisi wa mambo na wanadiplomasia wanatabiri kwamba kile kinachoonekana kama ni kulega kamba kwa Iran huenda kikawa ni mbinu tu ya taifa hilo ya kusogeza mbele muda na wala sio kusujudia mapendekezo ya nchi za magharibi.Iran inasema iko tayari kuingia kwenye mazungumzo kuhusu vishawishi vilivyotolewa lakini imekataa sharti la kukomesha shughuli zake za urutubishaji wa madini ya Uranium technologia ambayo inadhaniwa inatumika kutengenezea bomu la kinuklia.Kwa upande mwingine kumekuwepo na taarifa ambazo hazijathibitishwa kwamba pande hizo mbili zinaweza zikafikia makubaliano ambayo huenda Iran ikakubali kusimamisha urutubishaji wa madini ya uranium katika kiwango ilichofikia sasa na badala yake nchi sita za magharibi zitazuia kuiwekea vikwazo vipya Iran.Wakati huohuo Marekani inashikilia kwamba haiwezi kushiriki mazungumzo ya Nuklia kabla ya Iran haijakomesha urutubishaji wa madini yake ya Uranium.