1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ISLAMABAD:Benazir Bhutto kurejea nyumbani kama alivyopanga

12 Oktoba 2007
https://p.dw.com/p/C7Ga

Waziri MKuu wa zamani wa Pakistan Bi Benazir Bhutto anapanaga kurejea nchini mwake wiki ijayo baada ya kuwa uhamishoni tangu mwaka 1999.Kiongozi huyo wa zamani anashikilia kuwa anarudi ili kuanza kampeni za uchaguzi jambo ambalo Rais Pervez Musharraf hakubaliani nalo.Rais Musharraf kwa upande wake anatoa wito wa kuahirishwa kwa safari yake mpaka pale mahakama itakapotoa uamuzi wake kuhusu uhalali wa ushindi wake katika uchaguzi wa rais uliofanyika mwishoni mwa juma lililopita.

Bi Bhutto aliyekuwa waziri mkuu mwanamke wa kwanza katika taifa la kiislamu anatarajiwa kuwasili katika mji wa kusini wa Karachi tarehe 18 mwezi huu ikiwa ni siku moja baada ya mahakama kuu kuanza kusikiliza kesi ya kupinga uchaguzi huo iliyowasilishwa na upinzani.

Wiki jana Rais Musharraf wa Pakistan aliridhia kufutiwa mashataka ya ufisadi yanayomkabili Bi Bhutto jambo lililopelekea yeye kuenda uhamishoni.Hatua hii huenda ikasababisha makubaliano ya kugawana madaraka kati yao.

Kulingana na kura ya maoni raia wengi wa Pakistan wanapinga makubaliano ya aina hiyo. Waziri mkuu wa sasa wa Pakistan Shaukat Aziz alitangaza kuwa uchaguzi mkuu unapangwa kufanyika mwanzoni mwa mwaka ujao katika mwezi wa Januari.