1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ISLAMABAD:Pakistan yamuondolea mashtaka ya rushwa Bhutto

2 Oktoba 2007
https://p.dw.com/p/CBKj

Serikali ya Pakistan imesema kuwa imemuondolea mashtaka ya rushwa Waziri Mkuu wa zamani wa nchi hiyo anayeishi uhamishoni Benazir Bhutto.

Waziri wa reli wa nchi hiyo Sheikh Rashid Ahmed amesema kuwa Baraza la Mawaziri pamoja na maafisa wa juu wa serikali ya nchi hiyo wamekubaliana kumuondolea mashtaka hayo ya rushwa Bi Bhutto.

Bhutto amekuwa katika majadiliano kwa muda sasa na Rais Pervez Musharaff kuangalia uwezekeno wa kukubaliana juu ya kugawana madaraka.

Wakati huo huo Generali Musharraf amemteua mkuu wa zamani wa idara ya usalama ya nchi hiyo Luteni Generali Ashfaq Kayani kuwa mkuu mpya wa majeshi ya nchi hiyo baada ya uchaguzi wa Jumamosi ijayo.

Generali Musharaff amesema kuwa atang´atuka cheo cha ukuu wa majeshi iwapo atashinda uchaguzi huo.

Hatua hiyo imekuja siku moja baada ya wabunge 80 wa upinzani nchini humo kutangaza kujiuzulu wakipinga mipango ya Rais Pervez Musharraf kuwania tena urais katika uchaguzi mkuu wa Jumamosi ijayo.

Wabunge hao wamechukua hatua hiyo kupinga uhalali wa Generali Musharraf kuingia katika uchaguzi huo wakati akiwa na cheo cha ukuu wa majeshi wakisema kuwa ni kinyume cha sheria na katiba ya nchi hiyo.

Ijumaa iliyopita mahakama kuu ya Pakistan ilitoa hukumu ya kumruhusu Musharraf kuwania tena urais wakati akiwa na cheo cha ukuu wa majeshi.