1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

ISLAMABAD:Rufaa kupinga uteuzi wa Rais Musharraf zasikizwa tena

3 Oktoba 2007
https://p.dw.com/p/CBKX

Mahakama kuu nchini Pakistan inaanza tena kusikiliza hoja za kupinga harakati za Rais Pervez Musharraf za kuteuliwa tena baada ya kukwama kwa saa mbili pale jaji mmoja alipojiondoa.Jaji Sardar Raza Khan alijiondoa katika jopo la majaji tisa waliokuwa wakisikiliza rufaa za kupinga uchaguzi wa rais wa jumamosi.Hatua hiyo ilimlazimu Jaji mkuu kuteua jopo jipya la majaji.

Jaji Khan anasema kuwa alishaeleza mtazamo wake kuhusu kesi hiyo wakati mahakama kuu ilipofutilia mbali rufaa za awali za kupinga uchaguzi huo Ijumaa iliyopita.Jaji Khan ni mmoja wa majaji watatu waliopinga uamuzi huo.

Maombi hayo ya rufaa yaliwasilishwa na wapinzani wa Rais Musharraf dhidi ya uteuzi wake ambao ni Jaji mkuu wa zamani Wajihuddin Ahmad na Makhdoom Amin Fahim ambaye ni naibu mwenyekiti wa chama cha waziri mkuu wa zamani Benazir Bhutto.Wakati huohuo Rais Musharraf anatangaza kuwa yuko tayari kugawana madaraka na Waziri Mkuu wa zamani Bi Benazir Bhutto endapo chama chake kitapata viti vya kutosha bungeni katika uchaguzi ujao wa wabunge.Serikali inatangaza kuwa iko tayari kufuta mshataka ya rushwa yanayomkabili Bi Bhutto jambo litakalomwezesha kushiriki katika uchaguzi.

Bwana Musharraf anaahidi kujiuzulu kama kiongozi wa jeshi endapo atashinda uchaguzi.Hapo jana alimteua mkuu wa idara ya ujasusi wa zamani kama mrithi wake wa kijeshi.