1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel kuongeza uchunguzi juu ya shambulio la meli za misaada.

Halima Nyanza30 Juni 2010

Israel inaweza kuongeza jukumu la uchunguzi wake juu ya shambulio lililofanywa dhidi ya meli zilizokuwa zikipeleka misaada katika ukanda wa Gaza, kwa kuruhusu jopo lililoundwa kuchunguza kisa hicho kuwahoji mashahidi.

https://p.dw.com/p/O6aH
Waziri mkuu wa Usrael Benjamin Netanyahu anaweza pia kuitwa na jopo kutoa ushahidi wake juu ya shambulio dhidi ya meli za misaada zilizokuwa zikielekea Gaza.Picha: AP

Taarifa iliyotolewa na serikali ya Israel, imesema kiongozi wa jopo hilo la uchunguzi Jaji Jacob Turkel amewasilisha ombi kupanuliwa kwa uchunguzi huo kwa kuwawezesha mashahidi kutoa ushahidi wao baada ya kula kiapo.

Jopo hilo linaloongozwa na Jacob Turkel, Jaji mstaafu wa mahakama kuu ya Israel, lilianza uchunguzi wake siku ya Jumatatu na kwamba Waziri mkuu wa nchi hiyo Benjamin Netanyahu  na waziri wake wa ulinzi wanaweza pia kuitwa kutoa ushahidi wao kuhusiana na tukio hilo lililotokea Mei 31, ambapo raia tisa wa Uturuki waliuawa.

Kiongozi huyo wa jopo, amesema juukumu lao ni kuchunguza kama kuzingira kulikofanywa na jeshi la majini la Israel na msafara wa meli za misaada uliendana na sheria za kimataifa na pia uchunguzi ya kitendo cha waratibu wa msafara wa meli na washiriki wake.

Miongomi mwa wanaounda jopo hilo ni pamoja na mtaalamu wa Israel wa masuala ya sheria za kimataifa, mkuu wa zamani wa jeshi, pamoja na waangalizi wawili wa kigeni, ambao ni mshindi wa tuzo ya Nobel na mwanasheria wa Canada Ken Watkin, pamoja na David Trimble, mwanasiasa kutoka Ireland ya kaskazini, ambaye alisema kuwa wote wamejidhatiti kuona uchunguzi unakuwa wa kuwajibika na kutumai kuwa utaweza hatimaye kutoa mchango wa maana kwa amani.

Tukio hilo lilitia doa uhusiano kati ya Israel na Uturuki iliyo nchi ya kiislamu ambayo ni mshirika wake muhimu, ambapo toka kutokea kwa shambulio hilo ili muita nyumbani balozi wake pamoja na kufuta mazoezi ya pamoja ya kijeshi yaliyokuwa yakifanywa na taifa hilo la kiyahudi.

Israel iliamua kufanya uchunguzi huo baada ya nchi na jumuia mbalimbali duniani kulishutumu shambulio hilo, kwa kufikiria kwamba itapinga pendekezo la Umoja wa Mataifa la kufanyika kwa uchunguzi wa kimataifa.

Shambulio hilo lililofanya na makomando wa Israel, matokeo yake liliangazia vizuizi vilivyowekwa na Israel katika ukanda wa Gaza ambao unadhibitiwa na chama cha Hamas, hali ambayo pia ilisababisha kulegezwa kwa vizuizi hivyo.

Ikijitetea Israel ilisema kuwa makomando wake ambao walivamia moja ya meli zilizofadhiliwa na Uturuki kupeleka misaada Gaza, walikuwa wakitekeleza vizuizi vilivyowekwa kwa ajili ya kuzuia silaha zisiwafikie wapiganaji wakiislamu walioko katika eneo hilo na kwamba walifyatua risasi ili kujihami baada ya wanaharakati waliokuwa ndani ya meli hiyo kuwashambulia visu na marungu.

Mwandishi: Halima Nyanza(Reuters)

Mhariri:Abdul-Rahman