1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yakubali kuwaondoa wanajeshi wake, Ghajar.

17 Novemba 2010

Kijiji cha Ghajar kinachogombaniwa, kilinyakuliwa kutoka kwa Lebanon 2006

https://p.dw.com/p/QBOT
Wanajeshi wa Israel mpakani mwa Lebanon baada ya vita vya 2006.Picha: AP

Baraza la mawaziri linaloshughulikia usalama nchini Israel limeukubali mpango wa kuwaondoa wanajeshi wake kutoka kijiji kinachogombaniwa kwenye mpaka wa Lebanon. Udhibiti wa kijiji hicho utaachiwa kikosi cha walinda usalama cha Umoja wa Mataifa.

Katibu wa baraza hilo la mawaziri, Zvi Hauser, amesema leo kamati maalum inayoshughulikia suala la usalama, imeridhia kufuata pendekezo la Umoja wa Mataifa la kuwaondoa wanajeshi wake kutoka kaskazini mwa kijiji cha Ghajar. Hivi karibuni wanajeshi wengine wa Israel watatumwa kusini mwa kijiji hicho, mpakani mwa taifa hilo la Kiyahudi na Lebanon.

Israelische Panzer bei Manöver in den Golan Höhen
Israel ilinyakua milima ya Golan kutoka kwa Syria mwaka wa 1967.Picha: AP

Eneo la kaskazini mwa Ghajar liko nchini Lebanon, na sehemu nyingine iko katika eneo linalokaliwa na Israel katika milima ya Golan na lilinyakuliwa kutoka kwa Lebanon katika vita vya mwaka wa 2006. Kikosi cha wanajeshi wa Umoja wa Mataifa wanaolinda amani kwa muda nchini Lebanon watapiga doria mpakani.

Kikosi hicho cha Umoja wa Mataifa, UNIFIL, kimekuwa kikiipa Israel mbinyo ili iwaondoe wanajeshi wake kutoka kaskazini mwa Ghajar kulingana na uamuzi nambari 1701 wa baraza la usalama la Umoja huo ambao ulisitisha vita kati ya Israel na wapiganaji wa vuguvugu la Kishia la Hezbollah la Lebanon mwaka wa 2006.

Hatua hiyo ya Israel ilianza kudhihirika wiki iliyopita baada ya waziri mkuu, Benjamin Netanyahu, kulijadili suala hilo na katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban ki Moon, mjini New York, Marekani.

Awali Israel ilikuwa imedinda kukiacha kijiji hicho kidhibitiwe na wanajeshi wa Umoja wa Mataifa, kikidai kwamba wapiganaji wa Hezbollah wangeweza kupenya tena mpakani.

Kijiji cha Ghajar ambacho kina wakaazi 2,200 kiko katika eneo linalopakana na Lebanon, Syria na milima ya Golan ambayo Israel ilinyakua kutoka kwa Syria katika vita vya mashariki ya kati mwaka wa 1967. Hatimaye wakaazi wengi waliandikishwa kuwa raia wa Israel na sasa wana vitambulisho viwili vya Syria na Israel.

Wengi wao hawataki kijiji chao kigawanywe. Wakaazi 1,700 wanaishi upande wa Lebanon na wengine 500 wanaishi katika eneo la Israel la kijiji hicho.

Mwandishi: Peter Moss / AFP

Mhariri: Othman Miraji.