1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroIsrael

Israel yasema imefungua njia mpya kufikisha misaada Gaza

13 Aprili 2024

Israel imesema imefungua njia mpya ya kuingiza malori ya misaada ya chakula kwenye Ukanda wa Gaza ikitaka kuionesha jumuiya ya kimataifa kwamba imeongeza juhudi za kupeleka mahitaji muhimu kwenye eneo hilo.

https://p.dw.com/p/4eigM
Malori ya misaada ikiingia Gaza
Malori ya misaada ikiingia Gaza Picha: Israeli Army via AFP

Hata hivyo, Umoja wa Mataifa umesema kiwango cha misaada kinachoingizwa hakijamudu kupunguza madhila yanayowakabili Wapalestina kwa sababu ya changamoto za usambazaji zinazotokana na mapigano.

Miezi sita tangu kuanza kwa mapigano, zaidi ya watu milioni moja wanakabiliwa na kitisho cha baa la njaa hali inayozidisha mzozo wa kibinadamu kwenye Ukanda wa Gaza.

Mapambano kati ya vikosi vya Israel na wanamgambo wa Kipalestina bado yanaendelea bila ya kuwepo dalili ya kupatikana mkataba wa kusitisha mapigano.

Hapo jana, vikosi vya Israel viliwapiga risasi na kuwaua Wapalestina wawili kwenye eneo la Ukingo wa Magharibi na walowezi wa Kiyahudi walivamia vijiji kadhaa wakachoma moto majengo na magari.