1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

JAKARTA:Meli yazama na mlima Kelut wahofiwa kulipuka

19 Oktoba 2007
https://p.dw.com/p/C7EX

Meli moja inaripotiwa kuzama karibu na kisiwa cha Sulawesi na kusababisha vifo vya takriban watu 29 huku wengine wakiwa hawajulikani waliko.meli hiyo ndogo ya mbao ilizama alhamisi usiku kabla kuwasili mjini Baubau kusini magharibi mwa Sulawesi kwa mujibu wa msemaji wa wizara ya usafiri Bambang Ervan.

Kulingana na mkuu wa shirika la msaada la Msalaba Mwekundu Laode Hamdansyah maiti 29 zimeopolewa majini ila abiria 200 wanaripotiwa kuwa kwenye chombo hicho.

Uongozi bado unachunguza chanzo cha ajali hiyo ila huenda idadi kubwa ya abiria ilichangia .Hata hivyo hali ya hewa na bahari inaripotiwa kuwa shwari wakati huo.

Wakati huohuo polisi waliojihami wamewalazimisha wanakijiji kuondoka makazi yao yanayozunguka mlima mmoja wa volcano unaoshukiwa kulipuka wakati wowote.

Mlima Kelut ulio na urefu wa futi 5712 ulio takriban kilomita 90 kutoka mji wa Surabaya kisiwani Java umetangazwa kuwa huenda ukaripuka wakati wowote.

Takriban wanakijiji laki moja kumi na sita wameagizwa kuyahama makazi yao ila wengi wao wanakaidi amri hiyo kwa madai ya kulinda mali yao.