1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Japan: Wasiwasi waibuka kuhusu wanasayansi wa kigeni

Iddi Ssessanga
7 Julai 2023

Kesi ya madai ya uvujaji wa teknolojia inayomhusisha mtafiti wa China katika taasisi ya juu ya utafiti ya Japani "inapaswa kuwa kengele ya tahadhari" kwa serikali, wanasema wataalam.

https://p.dw.com/p/4TbIp
Illustration | Japan und China
Japan na mataifa ya Magharibi kama Marekani yamezidi kuwa na wasiwasi kuhusu uhamishaji wa teknolojia ya kisasa kwa China.Picha: daniel0Z/Zoonar/picture alliance

Quan Hengdao, mtafiti mkuu mwandamizi katika Taasisi ya Kitaifa ya Sayansi ya Juu ya Viwanda na Teknolojia (AIST), mjini Tsukuba, katika mkoa wa Ibaraki nchini Japani, alikamatwa hivi karibuni kwa tuhuma za kuvujisha data iliyopatikana kama sehemu ya kazi yake katika AIST kwa kampuni ya China, kinyume na sheria inayokataza ushindani usio wa haki.

Quan, 59, amefanya kazi katika taasisi hiyo tangu Aprili 2002 lakini pia akawa profesa katika Chuo Kikuu cha Teknolojia cha Beijing mwaka 2006, kulingana na uchunguzi wa gazeti la Sankei.

Chuo kikuu cha Beijing na Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Nanjing, ambapo alikuwa mwanafunzi, ni taasisi muhimu katika "Wana Saba wa Ulinzi wa Kitaifa," ikimaanisha kuwa zina uhusiano na jeshi la China.

Pia imeelzwa kuwa Quan alikuwa sehemu ya programu ya "Thousand Talents" ya serikali ya China, ambayo inalenga kuvutia watafiti katika nyadhifa muhimu ili kusaidia kuendeleza uwezo wa Beijing wa kisayansi na kiteknolojia.

Recycling im Panasonic Eco Technology Center in Kato in Japan
Japan ni mmoja ya mataifa yalioendelea zaidi katika nyanja ya teknolojia ya kisasa.Picha: Everett Kennedy Brown/dpa/picture-alliance

Mtafiti huyo anatuhumiwa kwa nini?

Quan anashutumiwa kutoa data za siri za teknolojia za kuunganisha misombo ya florini kwa mradi wa biashara nchini China ambao alianzisha na mkewe. Miezi michache baada ya data hizo kutumwa, kampuni ya wanandoa hao ilipata hati miliki ya teknolojia hiyo nchini Uchina.

Taarifa ambazo Quan alitoa "hazionekani kuwa zinazohusiana na ulinzi au teknolojia zinazohusiana na usalama wa kiuchumi," alisema Jin Matsubara, mwenyekiti wa zamani wa Tume ya Kitaifa ya Usalama wa Umma ambaye kwa sasa ni mwanachama wa Chama cha Kidemokrasia cha Kikatiba cha Japan, kituo hicho, chama cha siasa za mrengo wa kushoto ambacho ndoyo chama kikubwa zaidi cha upinzani katika bunge la Japan.

Soma pia: Marekani, Japan zakubaliana kuimarisha ushirikiano wa kiusalama

Lakini kesi hiyo inaangazia uharibifu unaoweza kusababishwa kwa Japan, alisema, na kuongeza kuwa "inapaswa kuwa kama kengele ya tahadhari" kwa serikali.

"Ni muhimu kutathmini kesi hii kwa mtazamo mpana," alisema. "Kuna malengo mawili ya sheria za Japani kuhusu sayansi na teknolojia; la kwanza ni kuzuia kupotea kwa teknolojia za hali ya juu na la pili ni kukuza mabadilishano ya kimataifa na kuwaalika watafiti wa kigeni wenye ujuzi na vipaji vya kipekee ili kushirikiana na wataalam wa Japan," Matsubara alisisitiza.

"Ndio maana kuna Wachina na Warusi wengi katika taasisi za utafiti na vyuo vikuu nchini Japan," aliiambia DW. "Watafiti hao wa kigeni wamekuwa muhimu sana kiasi kwamba taasisi zingine haziwezi kufanya kazi bila wao."

China na Marekni katika vita vya kibiashara

Vikwazo vya kushiriki teknolojia ya kisasa

Japani na nchi za Magharibi kama Marekani zimezidi kuwa na wasiwasi katika miaka ya hivi karibuni kuhusu uhamisho wa teknolojia ya kisasa kwenda China.

Utawala wa Rais wa Marekani Joe Biden ulisema unataka kuzuia teknolojia ya hali ya juu ya nchi za magharibi kununuliwa na vikosi vya jeshi la China na mashirika ya kijasusi. Mwaka jana, Washington iliweka vizuizi kwa China kupata chip za kisasa na vifaa vya kutengeneza chip, ikitoa sababu za usalama wa kitaifa.

Japan na Uholanzi pia hivi karibuni zilitangaza vikwazo vipya vya usafirishaji wa bidhaa kwenye teknolojia ya utengenezaji wa chipsi, bila kuitaja China.

Matsubara anadokeza kwamba masharti ya Sheria ya Kitaifa ya Ujasusi ya China yanawataka Wachina wote kutoa maarifa yote waliyopata ng'ambo kwa serikali, licha ya makubaliano yoyote ya kutunza siri ambayo wanaweza kuwa wametia saini.

Na hiyo ina maana kwamba "kila Mchina ana uwezo wa kuwa jasusi," aliongeza.

"Hii ndiyo sababu nchi kama Japan na Marekani hazina chaguo bali kuwatenga watafiti wa China kutoka taasisi zinazoshughulikia teknolojia nyeti sana za kiuchumi au zinazohusiana na usalama kupitia utumiaji mzuri wa mfumo wa kibali cha usalama," alisema.

Virusi vya Corona vyaambukiza wengi zaidi China

Majasusi wengi zaidi nchini Japani?

Wengine wanaamini kwamba serikali za Japan zilizofuatana zimeshindwa kuchukua tahadhari zinazohitajika na kwamba usalama wa taifa unahatarishwa.

Soma pia:Marekani na Taiwan zasaini makubaliano ya kibiashara 

"Sielewi jinsi Quan alivyoruhusiwa kubaki katika wadhifa huo kwa miaka 20 bila kuchunguzwa," alisema Yoichi Shimada, profesa wa uhusiano wa kimataifa katika Chuo Kikuu cha Jimbo la Fukui.

"Kwangu mimi, hii inaonyesha tu jinsi tulivyolegea linapokuja suala la mustakabali wa kiuchumi wa Japani na usalama wetu wa siku zijazo. Kwa kweli ni jambo lisilosameheka."

Shimada alisisitiza kuwa ana "hakika kuna majasusi wengi zaidi kutoka China na kwingineko" nchini Japan. Alitoa wito kwa serikali kutosubiri tena kushughulikia tatizo hilo.

"Hisia yangu ni kwamba serikali hii na vyuo vikuu wamekuwa dhaifu sana juu ya matatizo haya na hii imedhihirisha ukubwa wa tatizo," alisema.

Chanzo: DW