1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

JERUSALEM: Israel yakanusha madai ya kuishambulia Iran

8 Januari 2007
https://p.dw.com/p/CCcN

Israel imekanusha ripoti iliyotolewa na gazeti la Uingereza Sunday Times kwamba inapanga kuvishambulia viwanda vya kurutubishia madini ya uranium nchini Iran kutumia silaha za kinyuklia.

Gazeti hilo lilizinukulu duru za jeshi la Israel zikisema ndege mbili za jeshi la angani zisizokuwa na rubani zinafanya mazoezi ya kukilipua kiwanda cha Natanz, kusini mashariki mwa mji mkuu Tehran, kutumia vichwa maalumu vya nyuklia.

Lakini waziri wa mashauri ya kigeni wa Israel, Mark Regev, ameitupilia mbali ripoti hiyo akisema si sahihi. Regev aliwaambia waandishi wa habari kwamba Israel inaheshimu juhudi za kidiplomasia zinazofanywa na jumuiya ya kimataifa kuutanzua mzozo wa nyuklia wa Iran.

Waziri anayehusika na maswala ya uhamiaji, Zeev Boim, amesema, ´Ni vizuri kwamba Israel haitajihusisha na itaiunga mkono jumuiya ya kimataifa na juhudi zake za kuukomesha mpango wa nyuklia wa Iran.´

Iran kwa upande wake imeapa kuchukua hatua kali dhidi ya shambulio lolote katika viwanda vyake vya nyuklia.