1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Je,serikali inaruhusiwa kutaifisha benki?

P.Martin - (DPA)19 Februari 2009

Mada mojawapo ilioshughulikiwa na magazeti ya Ujerumani leo Alkhamisi ni mswada wa sheria itakayofungua njia kwa serikali kutaifisha taasisi zilizo katika hatari ya kufilisika.

https://p.dw.com/p/GxKc
** ARCHIV ** Die Zentrale der Hypo Real Estate - Bank, aufgenommen am 13. Feb. 2008 in Muenchen. Angesichts der juengsten Entwicklungen um den taumelnden Hypothekenfinanzierer Hypo Real Estate (HRE) fordern Politiker von Union und Gruenen den Ruecktritt von Vorstandschef Georg Funke. (AP Photo/Diether Endlicher) --- ** FILE ** A Feb. 13, 2008 file photo shows the Hypo Real Estate bank headquarters in Munich, southern Germany. (AP Photo/Diether Endlicher, File)
Makao makuu ya benki ya Hypo Real Estate mjini Munich.Picha: AP

Gazeti la MÜNCHNER MERKUR linauliza:

"Je,serikali au Kansela wa Ujerumani anaruhusiwa kutaifisha kampuni ya binafsi na kumuondosha mmiliki? Kwa maoni ya gazeti hilo jawabu ni ndio, anaruhusiwa na anapaswa kufanya hivyo ikiwa hakuna njia nyingine ya kuhifadhi uthabiti wa uchumi mzima-kwa mfano benki inayotoa mikopo ya nyumba Hypo Real Estate iliyo hatarini kufilisika.Kutaifisha benki kama hiyo wala haihusiki na Marx au Ujerumani ya Mashariki ya zamani,DDR. Bali anachokifanya Kansela kama mdhamini,ni kushughulikia tatizo hilo kwa maslahi ya umma."

Gazeti la SCHWÄBISCHE ZEITUNG likisitika linaeleza hivi:

"Pesa za walipa kodi zilizopindukia Euro bilioni 100 zimemiminiwa katika benki hiyo lakini wamiliki bado wanashindwa kuinusuru. Ikiwa benki hiyo itaruhusiwa kufilisika basi wamiliki hisa na wawekezaji watapata hasara kubwa mno.Wimbi hilo la hasara litaathiri pia taasisi zingine za fedha na kuhatarisha kiini cha uchumi wa taifa.Kwa hivyo serikali lazima ichukue hatua-na kwa sababu hiyo ipitishwe sheria itakayoruhusu benki hiyo kutaifishwa.Lakini ingekuwa bora zaidi kama isingekuwepo haja ya kutumia sheria kama hiyo." Hayo ni maoni ya SCHWÄBISCHE ZEITUNG.

Sasa tunageukia mada nyingine.Kampuni ya magari-Opel inayokabiliwa na kitisho cha kupunguziwa nafasi za ajira katika viwanda vyake nchini Ujerumani. Serikali ikizingatia kumiliki sehemu ya hisa za kampuni hiyo,gazeti la RHEIN-ZEITUNG linapinga fikra hiyo.Kwa maoni yake:

"Njia iliyo sahihi ni kuruhusu kiwanda kingine kuingilia kati kama mshirika mpya.Lakini tatizo ni kuwa hata makampuni mengine yanajikuta katika hali mbaya ya kiuchumi.Hapo ndio serikali inapopaswa kuchukua hatua-yaani itafute njia ya kuyawezesha makampuni mengine ya magari kuingilia kati kwa kuipatia mikopo itakayolipwa baadae."

Kwa kumalizia tunaitazama mada inayochomoza magazetini takriban kila siku - mgogoro wa fedha ulioathiri uchumi kila pembe ya dunia.Gazeti la EMDER ZEITUNG linasema:

"Hivi sasa mipango mbali mbali inapendekezwa kufufua uchumi ulioanguka nchini.Lakini raia wana mashaka yao kuhusu mipango hiyo kwani hawajui kilichokuwemo katika mipango hiyo na iwapo kweli itasaidia kukivuka kipindi hiki kigumu.Lengo la mipango ya kusaidia kufufua uchumi ni kuondosha hofu za umma na kurejesha imani yao-lakini hiyo si rahisi,kwani wanasiasa wametambua kuwa juhudi za kutaka kujenga imani hazitosaidia kushinda kura katika uchaguzi ujao."