1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Juhudi za kidiplomasia zashika kasi Mashariki ya kati.

Oummilkheir14 Oktoba 2007

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani amewasili Israel kwa mazungumzo yatakayomfikisha pia katika maeneo ya utawala wa ndani.

https://p.dw.com/p/C77o

Waziri wa mambo ya nchi za nje wa Marekani Condoleezza Rice amewasili Jerusalem hii leo katika juhudi za kuandaa mkutano wa kimataifa kuhusu amani ya Mashariki ya kati.Leo jioni bibi Condoleezza Rice atakutana na waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert.Leo usiku waziri huyo wa mambo ya nchi za nje wa Marekani atazungumza na waziri mkuu wa Palastina Salam Fayyad mjini Jerusalem kabla ya kukutana baadae na kiongozi wa utawala wa ndani Mahmoud Abbas.Wakati huo huo juhudi za kidiplomasia kati ya Israel na Palastina zimeshika kasi.Wawakilishi wa tume za Palastina na Israel wanapanga kukutana mara tatu,bila ya kutaja mazungumzo ya papo kwa papo kati wakuu wa tume zao ambao ni Ahmad Qorei aliyewahi kua waziri mkuu wa Palasatina na mkurugenzi wa ofisi ya waziri mkuu wa Israel Yoram TURBOWITZ.Jana mkuu wa tume ya Palastina mazungumzo Ahmad Qorei alizungumza na mjumbe wa Marekani David Welsh na kumuelezea umuhimu wa kutangazwa waraka timamu mwishoni mwa mazungumzo ya amani yatakayoitishwa mwezi ujao nchini Marekani.Wakati huo huo waziri mkuu wa Israel Ehud Olmert ameamua kumteuwa waziri wa mambo ya nchi za nje Tzipi Livni kuongoza ujumbe wa Israel katika mazungumzo ya amani ya mashariki ya kati mwezi ujao nchini Marekani.Kulingana na vyombo vya habari vya Israel,waziri mkuu Olmert huenda akatangaza uamuzi huo hii leo,wakati wa mkutano wa kila wiki wa baraza lake la mawaziri.Hadi wakati huu wahariri wa kisiasa nchini Israel walikua wakiamini ,kiongozi wa pili serikalini Haim Ramon angechaguliwa kuongoza ujumbe wa Israel mazungumzoni.Kuteuliwa bibi Tzipi Livni kunaashiria msimamo mkali unaoweza kufuatwa na Israel katika mazungumzo hayo .