1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Juhudi za kupambana na ugaidi nchini Nigeria

Oumilkher Hamidou22 Juni 2012

Jinsi mji wa kaskazini wa Nigeria Kano unavyojitahidi kurejesha hali ya kuaminiana miongoni mmwa jamii na waislam na wakristo,licha ya vitisho vya kigaidi vya Boko Haram

https://p.dw.com/p/15JcR
Ado Bayero Emir wa KanoPicha: Thomas Mösch

Mwishoni mwa mwezi wa Januari mwaka 2012 mji wa Kano ulijikuta ukikabwa na visa vya kigaidi. Wanamgambo wa kundi la itikadi kali la Boko Haram walivishambulia vituo kadhaa vya serikali. Walivurumisha mabomu na kuwapiga risasi askari polisi. Zaidi ya watu 180 waliuwawa- mji huo wa pili kwa ukubwa nchini Nigeria ukakumbwa na kihoro na maisha kujiinamia kutokana na marufuku ya watu kutoka nje usiku. Miezi michache baadae hali ya kawaida ingawa ya kutisha inatawala. Katika majimbo jirani magaidi wanafanya mashambulio dhidi ya makanisa na dhidi ya vikosi vya usalama. Wakaazi wa Kano wanajiuliza: Na wao yatawafika lini hayo?

Kano ni jiji la kale ambalo wakaazi wake ni waislamu, lakini tangu enzi za ukoloni malaki ya wahamiaji wa kikristo walihamia huko kutoka sehemu ya kusini ya Nigeria.Wengi wao wanaishi katika mtaa wa "Sabon Gari"- ikimaanisha "Mji Mpya". Mchana hali ya maisha ni ya kawaida- kuna vituo vichache tu vya uchunguzi. Maduka na masoko yanafunguliwa. Usiku njia zinakuwa tupu, watu wanafanya haraka haraka kurejea majumbani, huku wanajeshi na polisi wakianza ukaguzi wao kila mahala. Mbali na wa Igbo ambao ni wakristo, katika mtaa huo wa Sabo Gari wanaishi pia watu wa kabila la Yoruba kutoka eneo la kusini magharibi la Nigeria na ambao mara nyingi utakuta kuna waislamu pia. Mmoja wao ni Sadiq ambae ni mwanafunzi. Anasema kwa kuwa yeye ni muislamu, amekuwa hivi sasa akiangaliwa kwa wasiwasi na majirani zake wa kikristo."Linapohusika suala la dini, hapo waislamu tunakuwa tunadhaniwa vyengine. Ila kama watu wanaelewa. Wakristo wanaiangalia hali hii kwa miwani ya kidini. Waislam ndio wanaobeba jukumu la hali hii. Hawaelewi kwamba hawa ni magaidi wanaotaka kuichafua dini."

Bibi mmoja anajitaja kuwa ni mkristo wa kabila la Igbo. Anasomea katika chuo kikuu cha Abuja. Hapendelei sana kwenda kuitembelea familia yake huko Kano kwasababu watu wengi wameuhama mji huo."Inasikitisha. Marafiki, jamaa, watu ambao mtu hukutana nao hawako tena. Ingawa hali hivi sasa si ya wasi wasi sana, hata hivyo, lakini watu hawajisikii tena vizuri kuishi mjini Kano.

1
Askofu Ransom BelloPicha: Thomas Mösch

Wazee wake ni wafanyabiashara na biashara imeporomoka sana hivi sasa, ndio maana anasema wazee wake wanashindwa hata kumsaidia. Hata maingiliano na marafiki wa kiislamu yamevunjika, anasema.

Hata hivyo, kuna wengine wanaohisi hakuna sababu ya kuuhama mji wa Kano. Wanahisi wanaofanya mashambulio ni kundi la wachache lililolenga kufanya fujo nchini.

Askofu Ransom Bello wa kanisa la kiinjili na ambae ni mwenyekiti wa shirikisho la wakristo wa Nigeria-CAN- mjini Kano, ana maoni sawa na hayo. Anawatolea mwito hasa waumini wenzake wasalie Kano."Hakuna sababu ya kuondoka.Tunaamini hatari iko kila mahala. Ikiwa wakati wangu haujafika, hakuna atzakaeweza kuniuwa. Lakini hatuwezi kufanya chochote ikiwa watu wameshaamua kuuhama mji wa Kano. Ninaelewa.Tunaweza tu kuwasihi.Wengi wameshaondoka. Na huu ndio ukweli.

Bombenanschlag in Maiduguri Nigeria ARCHIVBILD 2012
Shambulio la bomu MaiduguriPicha: picture-alliance/dpa

Katika miaka ya hivi karibuni, uhusiano kati ya wakristo na waislamu umeboreka. Kinyume na zamani, hakuna maatumizi ya nguvu yaliyoshawishiwa kidini yanayotokea Kano. Na majadiliano kati ya jamii hizo mbili yameshika kasi ili kujiepusha na hatari iliyoko.

Hali bado si salama. Mashambulio yamepamba moto katika jimbo jirani la Kaduna ambako kundi la kigaidi la Boko Haram limechapisha ripoti na kuwaonya wakaazi wa Kano watahujumiwa ikiwa wataendelea kushirikiana na vikosi nvya usalama kupambana na magaidi.

Mwandishi:Mösch,Thomas (MMR Afrika)/Hamidou Oummilkheir

Mhariri: Miraji Othman