1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Juhudi za uokozi zinaendelea Pakistan

Kalyango Siraj29 Oktoba 2008

Ujerumani imeahidi msaada

https://p.dw.com/p/FjuI
Familia inampeleka kijana aliejeruhiwa katika hospitali ya mjini Quetta, PakistanPicha: AP

Juhudi za uokozi baado zinaendelea kufuatia tetemeko la ardhi kutokea mapema leo katika mkoa wa Baluchistan unaopakana na Afghanistan. Watu zaidi ya 150 wameuawa na wengine 15,000 kuachwa bila makazi.Wataalamu wanasema tetemeko hilo lilikuwa na nguvu za 6.4.

Huku juhudi hizo zikiwa zinaendelea,kuna habari kuwa kumetokea tetemeko lingine dogo katika eneo hilo moja katika mkoa wa Baluchistan ambalo liliharibiwa na tetemeko la asubuhi ya kuamkia jumatano.

Hakuna fununu za majeruhi ama hasara kutokana na tetemeko la pili ambalo limetokea saa 12 baada ya lile la mwanzo na kusikika katika mji wa Quetta pamoja na maeneo jirani nchini Pakistan na Afganistan.Maafisa wanasema tetemeko la pili lilikuwa la nguvu sawa kama lile la mwanzo la 6.4 katika kipimo cha Ritcher.

Tetemeko la pili lilileta hofu miongoni mwa wakazi wa maeneo hayo ambao walikimbilia maeneo ya wazi.Taarifa zaidi zinasema kuwa watu kadhaa walijeruhiwa katika purukushani hiyo kwani walikuwa mara wakiogongana na kukanyagana wakijaribu kuokoa maisha yao.

Idadi kamili ya waliokuwa inatatanisha.Hapo awali vyombo vya habari vikiwanukuu maafisa mbalimbali wa Pakistan vilisema kuwa walioariki walikuwa 160 na wengine 15,000 kuachwa bila makazi na nyumba 2,000 kuharibiwa kabisa.

Yeye mwenyeki wa mamlaka ya taifa inayoshughulikia majanga ya NDMA, mwanajeshi mstaafu,Luteni Generali Farooq Ahmed ameuambia mkutano wa waandishi habari kuwa kufikia wakati huo waliokufa 155 na waliojeruhiwa kufikia 300.

Lakini shirika la habari la AFP linasema kuwa meya wa mji wa Ziarat, ulioko umbali wa kilomita 50 kaskazini mwa Quetta,ameliambia kuwa idadi ya waiouawa imefikia 170.Aidha amesema kuwa watu 400 ndio wamejeruhiwa katika sehemu hiyo.Maafisa wanasema idadi ya wahanga inaweza kuongezeka kutokana na uharibifu uliotokea.

Wafanya kazi za kutoa misaada wameweza tu kufikia vijiji vya karibu na barabarakuu huku vingine vingi vilivyoko ndani havifikiki kutokana na uharibifu wa miundo mbinu.

Hii inatokana na tetemeko hilo kusababisha maporomoko ya udongo katika sehemu nyingi ambako barabara zikawa hazipitiki na hivyo kuzuia juhudi za watoaji misaada. Ndege za kijeshi za helikopta zilitumiwa kuona hali kamili ilivyo.Mkuu wa jeshi eneo hilo Meja Generali Asif Nawaz miongoni mwa mengine amesema kuwa jeshi limeweka kambi maalum za kuratibu shughuli za misaada.

Mamlaka ya kitaifa inayoshugulikia majanga NDMA pia nayo ilichukua hatua kwa kutuma shehena kadhaa za mahema,blanketi na nguo ngumu ili kuongezea shehena nyingine ya hema 3,000 ambazo tayari ziko Quetta.

Kwa muda huohuo Umoja wa Ulaya unasema uko tayari kutoa msaada wa kibinadamu kwa wahanga wa tetemeko hilo.Kamishna wa masuala ya nje wa Umoja huo,Benita Ferrero-Waldner,amesema jumatano kuwa ikiwa serikali ya Pakistan itaomba kusaidiwa bila shaka umoja huo utaitikia mara moja.

Ujerumani imetoa msaada wa pesa kwa utawala wa Islamabad.Wizara ya mashauri ya kigeni ya Ujerumani imesema kuwa Euro laki mbili unusu ambazo ni sawa na dola za kimarekani zaidi ya laki tatu zimetengwa ili kuweza kutumiwa kununulia vifaa vya msaada kama vile hema, blanketi pamoja na chakula.