1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
UchumiKimataifa

Jukwaa la Uchumi Duniani la Davos kuanza leo

15 Januari 2024

Mkutano wa Kimataifa wa Jukwaa la Kiuchumi duniani, WEF umeanza hii leo huku mizozo ya Mashariki, Ukraine, mabadiliko ya tabianhi pamoja na namna teknolojia ya kubuni inavyoathiri maisha yetu vikitarajiwa kuwa mada kuu

https://p.dw.com/p/4bFZa
Davos, Uswis | Viti vya wazungumzaji katika mkutano wa Jukwaa la Kiuchumi Duniani
Jukwaa la Kiuchumi la Dunia DavosPicha: Salvatore Di Nolfi/KEYSTONE/picture alliance

Orodha ya vipaumbele vya dunia imeongezeka katika mkutano wa mwaka huu wa Jukwaa la Kiuchumi la dunia, ambalo linawakutanisha viongozi wa biashara, siasa na wasomi wengine mjini Davos, Uswisi, unaoendelea hadi siku ya Ijumaa.

Zaidi ya wakuu 60 wa nchi na serikali, akiwemo Rais wa Israel Isaac Herzog na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyiy wako Davos kuhudhuria mkutano huo wakiwa miongoni wa wahudhuriaji zaidi ya 2800 wanaohusisha wasomi, wasanii na viongozi wa mashirika yasio ya kiserikali.

Kuelekea mkutano wa mwaka huu, shirika la hisani la Oxfam limetoa ripoti inayoonesha kuwa matajiri zaidi watano duniani watafikisha dola trioni moja.

Oxfam ambayo kwa miaka mingi imekuwa ikijaribu kuangaziatofauti inayoongezeka kati ya matajiri wakubwa na idadi ya watu ulimwenguni imesema kuwa, pengo hilo limeongezeka tangu kuzuka kwa janga la Uviko-19 mapema mwaka 2020.

Soma pia:Mada za Migogoro, tabianchi na AI kuugubika mkutano wa Davos

Shirika hilo limesema hayo wakati wa mkutano wa Jukwaa la uchumi la Dunia na kuongeza kuwa watu watano ambao ni matajiri zaidi ulimwenguni, Mkurugenzi Mtendaji wa Tesla Elon Musk, Bernard Arnault na familia yake ya kampuni ya kifahari ya LVMH, mwanzilishi wa Amazon Jeff Bezos, mwanzilishi wa Oracle Larry Ellison na gwiji wa uwekezaji Warren Buffett - utajiri wao umeongezeka kwa asilimia 114 mnamo 2020 wakatidunia ikipambana na janga la Uviko.

Oxfam: Huu ni muongo wa mgawanyiko

Mkurungenzi Mtendaji wa muda wa Oxfam Amitabh Behar amesema kuwa dunia inaingia muongo wa mgawanyiko ambapo mabilionea watano bora wameongeza utajiri wao mara mbili zaidi na kwa upande mwingine watu karibu bilioni tano wamekuwa masikini zaidi.

"Tunaita muongo wa mgawanyiko, umeona mabilionea wakiongeza karibu dola 3 trilioni kwenye utajiri wao." Alisema Behar,

Aliongeza kuwa wakati matajiri wakiongeza utajiri wao kwa upande mwingine, wafanyakazi milioni 800 ulimwenguni hawajaweza kuwa na mishahara ambayo inalingana na mfumuko wa bei.

Nchi tajiri kiuchumi zatakiwa kupunguza umasikini duniani

Kwa sasa Elon Musk anatajwa ndie mtu tajiri zaidi ulimwenguni ambapo kulingana na Oxfam ikitumia takwimu za  Forbes utajir wake unakaribia dola bilioni 250.

Aidha shirika hilo la oxfam limeongeza kuwa uvamizi wa Urusi nchini Ukraine umechangia pakubwa kuongeza gharama za maisha  ambapo ulisababisha mahitaji muhimu kupanda ikiwemo nishati na chakula hatua ilioathiri vibaya mataifa masikini.

Soma pia:Davos mjadala watawala ushirika wa China kimataifa

Katika Jukwaa hilo la Uchumi la Dunia huko Davos mada mbalimba zinatarajiwa kujadiliwa ikiwa ni pamoja na vita vya Gaza na Ukraine, lakini Ikulu ya Kremilin imesema kuwa mazungumzo hayo kuhusu mapendekezo ya amani ya Ukraine hayatafauluchochote kwani Urusi haikushiriki katika majadiliano hayo.

Jukwaa hilo ambalo hukusanya pamoja viongozi wa kisiasa na kibiashara na wengine wengi, itafunguliwa rasmi baadaye leo, na hotuba kuu za viongozi zitaanza hapo kesho ambapo Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken, Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron na viongozi wakuu wa Mashariki ya Kati wanatarajiwa kuhudhuria Kongamano hilo.