1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kabila anyoosha mkono wa diplomasia

31 Oktoba 2013

Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo amewataka wapiganaji wa makundi yote ya waasi mashariki mwa nchi yake kuweka silaha zao chini, baada ya kile kinachoaminika kuwa ni kusambaratika kwa kundi la M23.

https://p.dw.com/p/1A9Ur
Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Rais Joseph Kabila wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.Picha: Reuters

Akihutibia taifa hapo jana (tarehe 30 Oktoba) kwa njia ya redio na televisheni, mara tu baada ya jeshi la serikali kuuteka mji wa Bunagana, Rais Kabila alilipongeza jeshi hilo na wale Umoja wa Mataifa kwa kulirejesha eneo la Rutshuru mikononi mwa serikali.

Hata hivyo, Rais Kabila akasema pamoja na ushindi huo wa kijeshi, diplomasia na mazungumzo baina ya Wakongomani yataendelea.

“Ninasisitiza wito wangu kwa wapiganaji wa kundi lililofurushwa kwenye mitaa ya Nyiragongo na Rutshuru kutua silaha zao chini kwa ikhari yao wenyewe kulingana na pendekezo la Nchi za Maziwa Makuu. Kinyume cha kufanya hivyo tutalazimika kuwapokonya silaha kwa nguvu. Wito wa aina hiyo hiyo unatolewa pia kwa makundi mengine ya wapiganaji ya kitaifa, kusitisha hatua zote za kijeshi kutasababisha wao na wengine kufaidika na mpango wa kuingizwa katika maisha ya kawaida.” Amesema Rais Kabila.

Kabila azionya nchi jirani, makundi ya kigeni

Katika hotuba hiyo ya kwanza tangu taarifa za kusambaratika kwa kundi la waasi wa M23 mashariki kwa nchi hiyo, Rais Kabila aliyatahadharisha pia makundi ya wapiganaji ya kigeni yalioko nchini huko Kivu.

Wanajeshi wa Kongo wakipumzika baada ya vita vya kuwafurusha M23 mashariki mwa nchi hiyo.
Wanajeshi wa Kongo wakipumzika baada ya vita vya kuwafurusha M23 mashariki mwa nchi hiyo.Picha: Stephanie Aglietti/AFP/Getty Images

“Kuhusu makundi yaliosalia ya kigeni yakiwemo FDLR, LRA, ADF/Nalu na FNL yanayoendelea kutaabisha wakaazi wa Kivu ya Kusini na Kivu ya Kaskazini, ninayatahadharisha kutua chini silaha haraka sana. Vyenginevyo, makundi hayo yatapokonywa silaha kwa nguvu na yatachukuliwa hatua kama tunayoendesha hivi sasa.”

Katika hatua nyengine, Rais Kabila ametumia hotuba hiyo kuzionya nchi jirani,ambayo hakuzitaja jina, kwamba amani ya kudumu ya Kanda la Maziwa Makuu itatokana na utekelezwaji wa Mkataba wa amani wa Addis Ababa.

“Kwan nchi jirani, ninaziambia mara nyingine kwamba njia muafaka ya kuleta amani na ustawi wa ukanda huu, ni utekelezwaji wa dhati na kwa nia nzuri kwa Mkataba wa Amani wa Addis Ababa na vile vile Azimio Namba 2098 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Ninawahimiza kutekeleza wajibu wao kulingana na mkataba huo.”

Anyoosha mkono wa diplomasia

Rais Kabila amesema ijapokuwa ushindi wa kijeshi umepatikana, lakini juhudi za kidiplomasia na kisiasa zitaendelea.

Wanajeshi wa Kongo wakifurahia ushindi dhidi ya M23.
Wanajeshi wa Kongo wakifurahia ushindi dhidi ya M23.Picha: Carl de Souza/AFP/Getty Images

“Mtizamo wetu ni ule wa kutafuta suluhisho la mzozo wa Kongo kwa njia tatu: ya kijeshi, ya kisiasa na kidiplomasia. Na ndilo tunalofanya sasa. Ushindi wa kijeshi huko Kivu hauwezi kuvunja juhudi zingine za kisiasa na kidiplomasia.”

Kufuatia ushindi wa jeshi la Kongo dhidi ya waasi wa M23, Rais Kabila aliwapongeza wanajeshi na kusema wameungwa mkono na taifa nzima.

Vile vile, aliwapongeza wanajeshi wa Tanzania katika kazi wanayoifanya kwenye kikosi cha Umoja wa Mataifa na kutoa heshima zake na rambirambi za pole kwa familia ya wanajeshi wa Kongo na wale wa Tanzania waliopoteza maisha yao kwenye uwanja wa mapambano.

Rais Kabila alitoa wito wa kutokueko na ulipizaji kisasi baina ya Wakongomani.

Mwandishi: Saleh Mwanamilongo/DW Kinshasa
Mhariri: Mohammed Khelef