1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mzozo wa Rwanda/Ujerumani

Mtullya, Abdu Said12 Novemba 2008

Ujerumani imethibitisha kuwa itampeleka Kabuye Ufaransa.

https://p.dw.com/p/FtEZ
Rose Kabuye akiongozana na aliekuwa waziri wa mambo ya nje wa Marekani Madeleine Albright .Picha: AP

Licha ya serikali ya Rwanda  kuchukua hatua kali ya  kumfukuza balozi wa Ujerumani,  Ujerumani  itampeleka Ufaransa mkuu  wa itifaki wa Rwanda,Rose Kabuye aliekamatwa na polisi wa Ujerumani  kwenye  uwanja  wa ndege wa  Frankfurt  jumapili  iliyopita.

Msemaji wa  idara ya mashtaka ya mji wa Frankfurt  amethibitisha leo kuwa Rose Kabuye  atapelekwa Ufaransa baada ya mahakimu wa  Ujerumani kutoa hukumu hiyo.Na serikali ya Ujerumani  imesema  kuwa haina kipingamizi  katika hilo.

Rose Kabuye ambae ni  mkuu wa itifaki nchini  Rwanda alikamatwa  kufuatana na  msingi wa  waranti wa kimataifa uliotolewa na Ufaransa. Kabuye anatuhumiwa kuhusika na mauaji ya rais Juvenal Habyarimana  aliekuwa mhutu. Habyarimana  aliuawa  kutokana na ndege  aliyokuwa  amepanda kutunguliwa.

Ufaransa inasema kuwa mauaji hayo ndiyo yalikuwa  chanzo cha  maauji halaiki  yaliyotendeka  nchini Rwanda mnamo  mwaka 1994.

Watu hadi laki nane, watusi  na wahutu waliokuwa na mtazamo  wa  ukadirifu waliangamizwa.

Rais Paul Kagame wa Rwanda amesema  Ujerumani  imehujumu uhuru wa nchi yake  kwa kuchukua  hatua  ya kumkamata  bibi  Kabuye. Rais Kagame amesema hatua hiyo ni  kitendo cha cha ujuvi.


Serikali ya  Rwanda  imelipiza  kisasi kwa   kumfukuza balozi  wa Ujerumani nchini. Balozi  huyo ameambia kuondoka nchini  Rwanda  mnamo  muda  wa  saa 48.Rwanda pia imemrejesha  nyumbani balozi  wake kwa ajili  ya mashauriano.

Lakini serikali  ya Ujerumani  imesema   , haikuwa na njia nyingine ila kumkamata afisa   Kabuye katika  msingi  wa waranti wa   kimataifa uliotolewa na Ufaransa.


Msemaji wa wizara ya mambo ya nje ya Ujerumani Jens Plötner ameeleza kuwa polisi  ya Ujerumani  imemkamata Kabuye kisheria .

Lakini hatua ya kukamatwa mpambe  wa rais  Kagame, Rose Kabuye imesababisha hasira  nchini Rwanda. Maalfu ya wanyarwanda  wamefanya maandamano makubwa na kuenda kwenye ubalozi wa Ujerumani na kwenye ofisi  za radio Deutschewelle mjini Kigali.

Bibi Rose Kabuye amekanusha madai ya mauaji  na kuhusika na ugaidi.