1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kampeni za uchaguzi zimepamba moto hata magazetini

Oumilkher Hamidou10 Septemba 2009

Utaabiri wa maoni ya wananchi unabadilika badilika,bado kila kitu kinawezekana baada ya september 27 ijayo

https://p.dw.com/p/JZNF
Cheti cha kupiga kura katika uchaguzi mkuu wa mwaka huuPicha: DW

Homa ya uchaguzi imepanda nchini Ujerumani,siku 17 kabla ya uchaguzi mkuu.Na magazetini pia hali si nyengine.Wahariri hii leo wanazungumzia juu ya mabadiliko ya maoni ya umma kuelekea vyama vya kisiasa na kufichuliwa siri ya kisa kilichotendeka miaka 26 iliyopita katika enzi za kansela wa zamani Helmut Kohl.

Tuanze lakini na kampeni za uchaguzi na jinsi makadirio ya taasisi zinazochunguza maoni ya umma yanavyobadilika badilika.

Gazeti la "NEUE OSNABRÜCKER ZEITUNG" linaandika:

"Inazidi kubainika kwamba kila kitu kinawezekana uchaguzi mkuu utakapaoitishwa September 27 ijayo.Vyama ndugu vya CDU/CSU na kile kidogo cha kiliberali FDP ingawa viko mbele,lakini makadirio kwamba chama cha mrengo wa shoto Die Linke kinazidi kusonga mbele hayana budi isipokua kuwatia hofu wafuasi wa muungano wa nyeusi na manjano.Hali hiyo imesababishwa zaidi na mada zinazobishwa mfano wa nishati ya kinuklea , kinu cha kinuklea cha Gorleben na vita vya Afghanistan mada ambazo kawaida zinapandisha zaidi mori za wapiga kura wa mrengo wa shoto.Mijadala iliyoripuka kuhusu mada hizo inaweza kuwagutua wapiga kura zaidi.Haimaanishi lakini kwamba Oscar Lafontaine na Gregor Gysi watakalia viti serikalini.Hata hivyo chama che Die Linke chenye nguvu kinaweza hata kikiwa upande wa upinzani ,kushawishi shughuli za serikali mpya,tukitilia maanani ukweli kwamba nia ya kuunda serikali za muungano naiwe ya nyeusi na manjano au ya nyekundu-manjano kijani,haitoweza kutekelezeka.:

Gazeti la "Der neue Tag" la Weiden linaandika kuhusu utafiti wa maoni ya umma kwa vyama ndugu vya CDU/CSU na kile cha kiliberali cha FDP-muungano unaojulikana kama wa "nyeusi na manjano."

Wanasiasa wa vyama ndugu vya CDU/CSU na pia wale wa FDP wameshaanza kutetemeka.Wiki chache kabla ya uchaguzi mkuu September 27 ijayo,utafiti wa maoni ya umma unaonyesha kura zao zitapungua na kuwa chini ya asili mia 50 -hali inayokumbusha yale yaliyotokea mwaka 2005,vyama hivyo vilipoashiriwa kupata wingi wa kura kuweza kuunda serikali,ukweli wa mambo ukawa mwengine kabisa na kuibuka serikali ya vyama vikuu vya CDU/CSU/na SPD -FDP kikajikuta kikiendelea kukalia viti vya upande wa upinzani bungeni.Wazo kwamba kasheshe hiyo inaweza tena kutokea na kuendelea kwa miaka minne mengine ,haistahiki kumtia kishindo kiongozi wa FDP Guido Westerwelle.

Atomgegner protestieren gegen Castor Transport nach Gorleben, 10.11.08
Wapinzani wa nuklea waandamana dhidi ya kupelekwa takataka za kinuklea huko GorlebenPicha: AP

Mada yetu ya mwisho inatokana na kisa cha kinu cha kinuklea cha Gorleben.Inasemekana matokeo ya uchunguzi uliofanaywa miaka 26 iliyopita kuhusu kinu hicho yalifichwa na serikali ya kansela wa zamani Helmut Kohl.Gazeti la "Kieler Nachrichten linaandika.

Wiki mbili kabla ya uchaguzi mkuu imekuja julikana kwamba serikali ya Helmut Kohl,imeficha matokeo ya uchunguzi kuhusu takataka za kinuklea za kinu cha Gorleben.Hakuna yeyote anaeamini kisa hicho kimegunduliwa kwa nadra tuu .Waziri wa mazingira Sigmar Gabriel anataka kuitumia kadhia hiyo katika kampeni ya uchaguzi.Kansela Angela Merkel anatakiwa aelezee msimamo wake na kupinga yaliyofanywa na mtangulizi wake.Eti pamefanyika udanganyifu.Kana kwamba Angela Merkel,ambae wakati ule alikua bado upande wa pili wa ukuta,anabeba jukumu la uzembe katika kinu cha kinuklea cha Gorleben.

Mwandishi:Oummilkheir Hamidou/Dt.Zeitungen

Mhariri:M.Abdul-Rahman