1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kampeni zaanza Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo

28 Oktoba 2011

Kampeni za uchaguzi zimeanza rasmi leo katika Jamuhuri ya kidemokrasia ya Congo. Katika eneo la mashariki mwa nchi hiyo,furaha ya wagombea ubunge ni kwamba, wanaruhusiwa kufanya kampeni katika maeneo tofauti ya nchi hiyo

https://p.dw.com/p/130pp
Mwanamuzi katika mitaa ya KinshasaPicha: Claus Wischmann/Martin Baer/Edition Salzgeber

Siku ya leo ikiwa ilikubaliwa kwamba haitakuwa kama nyingine kutokana na kuanzishwa rasmi kwa kampeni za uchaguzi, raia wa Goma pamoja na baadhi ya miji mingine ya DRC, waliamka katika hali ya utulivu.

Katika redio mbalimbali za mahali, kunazo risalama mbalimbali za utulivu na usalama, kwa wagombea na pia kwa raia watakaochagua rais pamoja na wabunge Novemba 28.

Kampeni za uchaguzi zikiwa zimeanza rasmi, furaha ya wagombea katika wilaya za Walikale na Masisi, ni zile risala za viongozi wa wanamgambo wa Maimai katika wilaya hizo, haswa wilaya ya Masisi, kwamba wagombea wote wanao uhuru wa kutembelea maeneo yote yaliyo chini ya himaya yake.

Msemaji wa jeshi la serikali katika operesheni dhidi ya waasi katika mikoa ya Kivu ya kusini na kaskazini, kanali Ekenge Sylvain, akizungumza na redio ya Umoja wa mataifa nchini DRC, OKAPI, alisema kwamba waasi pamoja na wanamgambo hawana chaguo jingine, isipokuwa kusalimisha silaha pasipo masharti yoyote.

Kanali Ekenge alitamka hayo, baada ya kutangaza kwamba kamanda mmoja wa Maimai ameuawa katika mapambano dhidi ya wapiganaji wake na jeshi la serikali katika wilaya ya Lubero kilometa 200 hivi kaskazini mwa mji wa Goma.

Kadhalika msemaji huyo wa jeshi la serikali katika mikoa ya kivu ya kusini na kaskazini, aliwaonya viongozi wa waasi iwe wa makundi ya wana Congo kama vile ya kigeni, kwamba wote watauawa kama kamanda Gervais Mwenyeudongo, kiongozi wa Maimai alieuawa Jumatano iliyopita, baada ya kuwashambulia wanajeshi wa serikali katika wilaya ya Lubero, na kuwateka nyara askari polisi.

Nao polisi wa mji wa Kisangani, katika mkoa wa Mashariki waliandamana katika mitaa ya mji huo hapo jana, kuonesha uwezo walio nao, wa kulinda usalama katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi.

Mwandishi: Kanyunyu, John
Mhariri: Josephat Charo