1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kampuni hewa, ufisadi na ukuwaji uchumi Afrika Mashariki

26 Mei 2014

Takwimu za mashirika ya fedha duniani zinaonesha kwamba eneo la Afrika ya Mashariki linakuja juu kiuchumi na kwamba huenda likawa kituo kikuu cha ukuwaji wa uchumi katika Afrika iliyo chini ya jangwa la Sahara.

https://p.dw.com/p/1C6m3
Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya ameidhinisha malipo yenye utata kwa kampuni mbili za Anglo Leasing.
Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya ameidhinisha malipo yenye utata kwa kampuni mbili za Anglo Leasing.Picha: Simon Maina/AFP/Getty Images

Hata hivyo, uwepo wa ufisadi mkubwa uliotitia katika eneo hilo unatishia ukuwaji wenyewe wa uchumi, na pia ongezeko la ukosefu wa usawa, na mambo yanayotakana nayo - kama vile uhalifu wa kawaida na hata ugaidi.

Mfano wa kashfa kubwa za kifisadi ambazo zimekuwa zikiandama nchi za eneo hilo ni kama ile ya Anglo-Leasing ya Kenya au za IPTL, Dowans, EPA, na hivi majuzi ya akaunti ya Escrow nchini Tanzania. Haya ndiyo mataifa mawili makubwa miongoni mwa mataifa matano yanaounda sasa kanda ya Afrika ya Mashariki.

Mifano ya kashfa hizo inaonesha kwamba serikali zimekuwa zikichuma kwa mkono mmoja, na kuzila fedha hizo kwa mkono mwengine kupitia mkururo wa kampuni za ukweli na uongo ambazo hupatiwa tenda za mabilioni ya fedha.

Yanapobainika hayo, serikali hizi hujidai kuja juu kuchukua hatua, lakini kampuni hizo huja juu kuelekea mahakamani ambako mara kadhaa serikali hushindwa na matokeo yake kampuni zikaendelea kufaidi fedha ya walipa kodi.

John Githongo, afisa wa serikali ya Kenya aliyefichua kashfa ya Anglo Leasing.
John Githongo, afisa wa serikali ya Kenya aliyefichua kashfa ya Anglo Leasing.Picha: picture-alliance/ dpa/dpaweb

Tunajiuliza chimbuko la kampuni za aina hii? Ni zipi nguvu zake? Na je, ni kweli serikali za eneo la Afrika ya Mashariki zina udhaifu huo kwenye mihimili yake ya kisheria kiasi ya kwamba mara nyingi hubwagwa mahakamani kwenye kesi za namna hii? Kubwa kuliko yote: Je, Afrika ya Mashariki bila ya ufisadi inawezekana?

Washiriki:

1. Mbunge David Kafulila kutoka Tanzania, ambaye hivi majuzi tu aliibua kile kilichopewa jina la kashfa ya akaunti ya Escrow, ambayo inatajwa kumeza shilingi bilioni 200. Tayari Ofisi ya Mkaguzi wa Serikali na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini humo zinasemekana kuanza kazi ya kuchunguza madai hayo.

2. Koigi Wamwere kutoka Kenya, ambaye aliwahi kuwa waziri msaidizi anayeshughulikia mawasiliano na habari katika serikali ya chama cha NARC, ambayo iliingia madarakani kwa kaulimbiu ya kulimaliza kabisa suala la kashfa ya Anglo-Leasing kwa kuwafikisha wahusika kwenye mikono ya sheria. Lakini serikali hiyo chini ya Rais Mwai Kibaki ikamaliza muda wake bila ya kuchukua hatua ya maana na matokeo yake hivi majuzi Rais Uhuru Kenyatta akaagiza deni la shilingi bilioni 1.4 linalodai kampuni mbili za Anglo Leasing lilipwe. Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Hazina wa Kenya, Kamau Thugge, tayari deni hilo lilishalipwa tangu tarehe 19 Mei mwaka huu wa 2014.

3. Foum Kimara kutoka Uingereza, ambaye ni mwanaharataki na mchambuzi wa masuala ya kiuchumi na kijamii, ambaye amekuwa akifuatilia na kuandika sana juu ya mapungufu ya kimfumo katika eneo la Afrika ya Mashariki.

Muongozaji: Mohammed Khelef
Mhariri: Josephat Charo