1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kansela Merkel amaliza ziara ya Afrika

8 Oktoba 2007

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel ameahidi kuongeza misaada ya maendeleo kwa Liberia sambamba na kuunga mkono kampeni ya kuifutia madeni nchi hiyo. Kansela Merkel amesema hayo katika kituo cha mwisho cha ziara yake barani Afrika.

https://p.dw.com/p/C77z
Angela Merkel barani Afrika
Angela Merkel barani AfrikaPicha: picture-alliance/dpa

Bibi Merkel ametoa ahadi hiyo nchini Liberia baada ya mazungumzo na rais Ellen Johnson Sirleaf wa nchi hiyo. Amesema ziara yake nchini Liberia ilikuwa na lengo la kutoa ishara ya kumwuunga mkono rais Ellen Johnson Sirleaf anaekabiliwa na changamoto ya kuijenga upya nchi yake baada ya vita vya miaka 14.

Bibi Merkel amesema Ujerumani itaongeza misaada yake ya maendeleo kwa Liberia na pia itaunga mkono kampeni ya kuifutia madeni nchi hiyo

Ameeleza kuwa Ujerumani inapendelea kuona Liberia ikisonga mbele katika ujenzi wa uchumi wake na ndiyo sababu kwamba inafanya kila linalowezekana ili madeni ya nchi hiyo yafutwe. Lakini matayirisho zaidi yatahitajika kwenye mkutano wa shirika la fedha la kimataifa IMF, ili kuzihimiza nchi nyingine nazo ziisaidie Liberia.

Bibi Merkel Merkel amesema sera za nje za Ujerumani zinaelekezwa katika juhudi za kupambana na umasikini. Lakini sera hizo pia zinaelekezwa katika kupiga vita rushwa, kupambana na udhalimu, ukiukaji wa haki za binadamu na uongozi mbaya barani Afrika.

Sambamba na kuahidi kutoa misaada zaidi kiongozi huyo wa Ujerumani amesema kuwa misaada hiyo kutoka nchi za magharibi peke yake haitatosha. Ameeleza kuwa ni bara la Afrika lenyewe linalowajibika kufanikisha juhudi za kupambana na umaskini na maradhi.

Katika ziara yake barani Afrika Kansela wa Ujerumani pia alizitembelea Ethiopia na Afrika Kusini ambapo alikutana na kiongozi jarabati, mzee Nelson Mandela .Bibi Merkel pia alifanya mazungumzo na rais Thabo Mbeki.