1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kanzela Merkel ampendekeza Christian Wulff kuwa Rais wa Ujerumani.

4 Juni 2010

Mrithi wa Rais Horst Köhler:

https://p.dw.com/p/NhuY
Merkel (Kushoto) na Rais mpya Wulff ?Picha: AP

Waziri-mkuu wa mkoa wa Lower Saxony, Christian Wulff,ndie anaetazamiwa kuwa Rais mpya wa Ujerumani.Hii ni kwa muujibu wa maafikiano kati ya vyama-tawala vya CDU/CSU na FDP waliofikia jana.

Vyama vya upinzani vya SPD na walinzi wa mazingira KIJANI, wameukosoa uteuzi huo wa mwanasiasa huyo wa chama cha CDU mwenye umri wa miaka 50. Siku 3 baada ya kujiuzulu rais Horst Köhler, Kanzela Angela Merkel,hakukawia kumpendekeza mtetezi wa vyama-tawala CDU/CSU na FDP nani mritjhi wake kwa wadhifa huo wa urais.

ANGELA MERKEL

"Tungependa hii leo kumpendekeza Christian Wulff, kushika wadhifa wa Rais wa Ujerumani.Christian Wulff , daima ni mtu mwenye kiu cha kuwaelewa wanadamu wenzake ,apendae kuonja kitu kipya,mvumbuzi na anaewanyoshea watu mkono.Hivyo, ndivyo nilivyomuelewa tabia yake wakati wa Muungano wa nchi mbili za Ujerumani.

Wakati huo huo, Christian Wulff, ni mtu mwenye mfumo wa kutathmini mambo na kutoa muongozo mkondo gani ufuatwe.Kwa jicho hilo, nahisi ni mtu barabara kuwa rais wa Ujerumani."

WAZIRI WA NJE WESTERWELLE:

Hata makamo wake na waziri wa nje Guido Westerwelle, alisifu ushirikiano mzuri na Bw.Wulff ambae katika mkoa wake wa Lower Saxony, anaongoza serikali ya muungano na chama cha waliberali cha FDP.Mwanasheria Wulff,halkadhalika, alipongezwa mno na mshirika 3 katika serikali ya muungano chama cha CSU.

KURA ZA KUTOSHA BUNGENI:

Kwahivyo, kuchaguliwa rasmi kwa Bw. Christian Wulff, Bungeni hapo Juni 30, ni uhakika,kwani vyama-tawala vina wingi alao wa viti 20.

Bw.Wulff mwenye umri wa miaka 50,ni mtu mwenye imani ya Kanzela Merkel, siasa zake ni kuleta maskizano na maelewano,mwenye busara na mtulivu.Kwa muda wa miaka mingi,Bw.Wulff, akipendeza kwa wananchi na akionekana ni mtu ambae angeweza kuwa kanzela wa Ujerumani.Lakini, alikuja kusema kwamba, hana nia wala ari ya kushika wadhifa huo.

Kwa mabadiliko haya ya Bw.Wulff, kushika wadhifa wa urais ambao hauna madaraka ya utendaji, bibi Angela Merkel, amemuondoa mpinzani mkali chamani ambae angeweza kushindana nae kugombea tena wadhifa wa ukanzela.

"Naamini yawezekana kuwaunganisha watu,kuchangia kidogo kuiunganisha jamii na hata kuwapa matumaini nyakati za shida."

Alisema Bw.Christian Wulff, anaetazamiwa sana kuwa rais mpya wa Ujerumani.

Mwandishi: Grässler,Bernd (DW Berlin)

Mtayarishi: Ramadhan Ali

Imepitiwa na :Hamidou Oummilkhei