1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kazi bado Bundesliga, ingawa bingwa ashabainika

18 Mei 2017

Bingwa wa ligi kuu ya Ujerumani, Bundesliga tayari ashajulikana ingawa nafasi ya mwisho ya moja kwa moja ya kucheza ligi ya vilabu bingwa msimu ujao pamoja na nafasi za kushiriki ligi ya Ulaya, zitajulikana Jumamosi.

https://p.dw.com/p/2dCII
1. Bundesliga 32. Spieltag |  Borussia Dortmund v TSG 1899 Hoffenheim - Bundesliga
Picha: Getty Images/Bongarts/M. Hitij

Siku hiyo ndipo raundi ya mwisho ya mechi za Bundesliga zitakapochezwa.

Bayern Münich waliunyakua ubingwa wa Bundesliga huku kukiwa kumesalia mechi tatu msimu kufikia kikomo. Darmstadt na FC Ingolstadt tayari wameshushwa daraja na Stuttgart na Hannover huenda wakachukua nafasi zao kutoka kwenye ligi ya daraja la pili.

Borussia Dortmund na Hoffenheim wanatazamia kujiunga na Bayern Munich katika kufuzu moja kwa moja katika ligi ya vilabu bingwa msimu ujao kwa kumaliza katika nafasi ya tatu. Timu itakayomaliza katika nafasi ya nnne basi italazimika kushiriki mechi za mchujo ili ifuzu kwenye ligi hiyo ya mabingwa wa Ulaya msimu ujao.

Wakiwa sawa kialama, Dortmund watakuwa wanakwaana na Werder Bremen nao Hoffenheim wavae njuga kucheza na Augsburg. Augsburg wao bado hawajafahamu hatma yao kwa kuwa alama walizo nazo zinaifanya kuwa mojawapo ya timu ambazo huenda zikashiriki mechi ya mchujo ya kuwania kusalia katika Bundesliga msimu ujao. Kwa sasa timu ambayo inaishikilia nafasi hiyo ya kucheza mechi ya mchujo ni Hamburg SV.

Mainz, Augsburg na Wolfsburg wote wako alama 2 pekeyake mbele ya Hamburg na tofauti ya baina yao ni bao moja tu. Mechi itakayoamua bila shaka itwakua ile hamburg wakiwa nyumbani dhidi ya Wolfsburg, ambapo Hamburg ni sharti watoe ushindi katika mpambano huo. Hata ikiwa Wolfsburg watabwagwa na Hamburg huenda wakanusurika kushuka daraja iwapo lakini wapinzani wake watashindwa kwa mabao mengi. Mainz watakuwa wanatoana jasho na Cologne inayofukuzia nafasi ya mwisho ya ligi ya Ulaya.

Fußball: Bundesliga FC Schalke 04 - Hamburger SV
Hali bado ni tete kwa HamburgPicha: Picture alliance/dpa/I. Fassbender

Hertha Berlin ambayo kwa sasa inaishikilia nafasi ya tano, inaweza kufuzu kwenye ligi ya Ulaya pia kwani ina alama moja mbele ya Freiburg itakayokuwa inacheza mechi ya mwisho dhidi ya mabingwa Bayern Münich, na hao Berlin wana alama tatu zaidi ya Cologne.

Werder Bremen huenda wakajipenyeza katika ligi ya Ulaya iwapo lakini, watailaza Dortmund na Freiburg wapoteze mechi yao kisha FC Cologne wawafunge Mainz.

Mwandishi: Jacob Safari/APE

Mhariri: Bruce Amani