1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kenya kufunga kambi za wakimbizi

7 Mei 2016

Serikali ya Kenya imesema itazifunga kambi mbili kubwa za wakimbizi kutokana na ukosefu wa usalama na changamoto za kiuchumi mpango ambao unashutumiwa na mashirika ya haki za binaadamu.

https://p.dw.com/p/1IjeI
Picha: Oli Scarff/Getty Images

Katibu wa kudumu katika wizara ya mambo ya ndani Karanja Kibicho amesema hapo Ijumaa kufungwa kwa kambi hizo kutakua na taathira mbaya na kwamba jumuiya ya kimataifa inapaswa kuchukuwa hatua za kuwajibka kwa pamoja kwa mahitaji ya kibinadamu yatakayozuka.

Serikali imeifura idara ya Masuala ya Wakimbizi ambayo inafanya kazi kwa kushirikiana na mashirika ya misaada kushughulikia maslahi ya wakimbizi.

Kibicho amesema utekelezaji wa mchakato wa kuwarudisha wakimbizi nyumbani kwa hiari uliofikiwa katika makubaliano kati ya Shirika la Kuwahudumia Wakimbizi la Umoja wa Mataifa , serikali ya Kenya na serikali ya Somalia hapo mwaka 2013 umekuwa wa kuburuza miguu mno.

Amesema Kenya imekuwa ikiwahifadhi wakimbizi hao kwa miaka 25 jambo ambalo limekuwa na athari zake kwa nchi hiyo.

Dadaab na Kakuma ndio zinazolengwa

Kambi zinazolengwa kufungwa ni ya Dadab na Kakuma. Dadaab ambayo iko mashariki mwa Kenya ndio kubwa kabisa ikiwa na wakimbizi zaidi ya 328,00 wengi wakiwa ni Wasomali wanaoukimbia mzozo katika nchi yao iliokumbwa na vita ambayo inapambana kuushinda uasi wa kundi la Al-Shabab lenye mahusiano na mtandao wa Al-Qaeda. Kambi ya Kakuma ina wakimbizi 190,000 wengi wao wakiwa ni Wasudani wanaokimbia vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini mwao.

Kambi ya wakimbizi ya Dadaab ambayo ndio kambi kubwa kabisa ya wakimbizi duniani.
Kambi ya wakimbizi ya Dadaab ambayo ndio kambi kubwa kabisa ya wakimbizi duniani.Picha: imago/Xinhua

Kibicho amesema kambi hizo zimekuwa zikilea magaidi kutoka kundi la Al-Shabab ambalo limekula kiapo cha kuishambulia Kenya kwa hatua yake ya kutuma vikosi Somalia kupambána na wanamgambo ikiwa ni sehemu ya kikosi cha Umoja wa Afrika kuipa nguvu serikali dhaifu ya Somalia.

Washambuliaji wawili katika duka kubwa la Westgate mjini Nairobi hapo Septemba 21 ambapo watu 63 waliuwawa walikuwa wakiishi katika kambi ya Kakuma.

Hii sio mara ya kwanza kwa Kenya kutishia kuwarudisha nyumbani wakimbizi na mashirika ya haki za binaadamu ya kimataifa yamelaani mpango huo.

Mashirika ya haki za binaadamu yalaani

Shirika la Human Rights Watch lenye makao yake nchini Marekani limesema maafisa hawakutowa ushahidi wa kuaminika wenye kuwahusisha wakimbizi hao wa Somalia na shambulio lolote la kigaidi nchini Kenya.Shirika hilo limesema halijuwi juu ya kutiwa hatiani kwa wakimbizi wa Somalia kwa kuhusika na shambulio lolote lile la kigaidi nchini Kenya.

Shirika la Amnesty lenye makao yake nchini Uingereza limesema hatua hiyo ni ya ovyo na inaweza kupelekea kurudishwa nyumbani kwa nguvu kwa wakimbizi hao katika nchi ambapo maisha yao bado yanaweza kuwa hatarini.

Kambi ya wakimbizi ya Kakuma.
Kambi ya wakimbizi ya Kakuma.Picha: picture-alliance/dpa

Muthoni Wanyeki kiongozi wa Amnesty wa kanda amesema "wakati ni kweli kuwapatia makaazi mapya katika nchi za tatu utekelezaji wake umekuwa wa mwendo wa pole mno, Kenya yenyewe inapaswa kufikria utatuzi wa kudumu wa suala hilo kwa kuwajumisha kikamilifu wakimbizi hao katika jamii ambao baadhi yao wamekaa Kenya kwa zaidi ya vizazi. Amesistiza kwamba "Kuwarudisha kwa nguvu katika hali ya ukandamizaji au mizozo sio chaguo."

Shirika la Madaktari wasio na Mipaka limesema kufungwa kw akambi hizo kutaharisha maisha ya zaidi ya Wasomali 330,000 na kutwakuwa na madhara mbaya sana ya kibinaadamu ya kuwarudisha watu kwa nguvu katika nchi iliokumbwa na vita wakiwa na nafasi ndogo ya kupatiwa msaada muhimu wa matibabu na wa kibinaadamu.

Mkuuwa shirika hilo kwa Kenya Liesbeth Aelbrecht ameitaka serikali kufukiria upya wito wao huo na kwa kushirikiana na mashirika ya misaada ya kibinadamu ambayo tayari yako katika kambi hizo kuendelea kutowa misaada ya kibiaadamu na kuhakikisha kuwepo kwa mazingira ya kuishi ya kukubalika kwa mamia na maelfu ya watu wenye mahitaji hayo makubwa.

Mwandishi : Mohamed Dahman/AP

Mhariri :Abdu Mtullya