1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kesi ya Thomas Lubanga yafunguliwa The Hague

A.Göbel - (P.Martin)26 Januari 2009

Hakuna hakika iwapo kesi za uhalifu wa vita husaidia kuponesha majeraha ya vita vya wenyewe kwa wenyewe au kuleta upatanisho hasa nchini Jamhuri ya Kongo ambako mapigano yangali yakiendelea mashariki mwa nchi hiyo.

https://p.dw.com/p/GgKb
The first suspect of the International Criminal Court, Congolese warlord Thomas Lubanga, left, adjusts his headset as his lawyer Jean Flamme of Belgium is seen right, at the start of the trial in The Hague, Netherlands, Monday March 20, 2006. Lubanga was arrested on three counts of war crimes and was flown to the Netherlands last Friday. (AP Photo/Peter Dejong)
Mshstakiwa Thomas Lubanga.Picha: AP

Hata hivyo leo hii Thomas Lubanga aliekuwa kiongozi wa wanamgambo wa Union of Congolese Patriots-UPC amefikishwa mbele ya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Vita ICC mjini The Hague kwa mashstaka ya kuwatumia watoto kupigana katika vita vya wenyewe kwa wenyewe mashariki mwa Kongo.

Hiyo ni kesi ya mwanzo ya kihistoria ya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu wa Vita(ICC).Thomas Lubanga anakabiliwa na mashtaka ya kuwaandikisha watoto kupigana katika vita vya kikabila katika wilaya ya Ituri mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo kati ya Septemba mwaka 2002 na Agosti 2003.Lubanga katika mwaka 2002 kwa kushirikiana na wanajeshi wa Uganda aliuteka mji wa Bunia wilayani Ituri.Inasemekana kuwa zaidi ya watu 8,000 waliuawa katika vita hivyo na zaidi ya watu laki tano walifukuzwa makwao.

Wapiganaji wengi katika jeshi binafsi la Lubanga walikuwa watoto kama anavyoeleza mwanasheria Franck Mulenda anaewawakilisha watoto watatu waliopigana katika jeshi hilo.

"Ndio ni uhalifu wa kivita-kuwateka nyara na kuwaandikisha watoto walio chini ya miaka 15 kama wapiganaji.Hayo ni matokeo yanayohusiana na mzozo wa kijeshi."

Akiendelea zaidi Mulenda anasema,wanamgambo wa Lubanga waliwavizia watoto waliokuwa njiani kwenda shuleni au kuteka maji.Mara nyingi watoto hao walilazimishwa kuua familia zao na kwa njia hiyo kuwavunja moyo na kuwafanya wawe makatili.Na wasichana wengi walibakwa wengine wakiwa na kama miaka kumi tu.Lakini Lubanga hasa anashtakiwa kwa ukiukaji mkubwa wa sheria ya Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu yaani kuwatumia watoto vitani kama wapiganaji.

Mawakili wanawawakilisha watoto 93 katika kesi hii ya Lubanga, mjini The Hague.Shahidi wa kwanza aliepigana kama mtoto katika jeshi la Lubanga anatazamiwa kusimama mahakamani siku ya Jumatano.Miongoni mwa mashahidi 34,kuna watoto waliokuwa wapiganaji hapo zamani na vile vile wanamgambo wa zamani waliohusika katika mapigano ya Ituri.

Lubanga alieongoza wanamgambo wa kabila la Hema kupigana dhidi ya watu wa kabila la Lendu anatazamiwa kukanusha mashtaka ya kutumia watoto chini ya umri wa miaka 15 kama wapiganaji katika jeshi la chama chake cha UPC kati ya mwaka 2002 na 2003.Yeye anadai kuwa alipigana kama mzalendo kuwazuia waasi na wapiganaji wa kigeni kupora mali asili ya Kongo katika eneo la Ituri mashariki mwa nchi.