1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

KHARTOUM: Bashir akanusha madai dhidi ya serikali yake

20 Machi 2007
https://p.dw.com/p/CCH8

Rais wa Sudan, Omar el Bashir, amekanusha madai kwamba serikali yake imehusika katika vitendo vya ukiukaji wa haki za binadamu katika jimbo la Darfur.

Mwezi uliopita muongoza mashtaka mkuu wa mahakama ya kimataifa ya uhalifu wa kivita mjini The Hague Uholanzi, Luis Moreno Ocampo, alimtaja waziri wa mambo ya ndani wa Sudan, Ahmed Mohamed Harun, na kamanda wa waasi, Ali Muhammad Ali Abdal Rahman, kama washukiwa wa kwanza wa uhalifu wa kivita katika jimbo la Darfur.

Hata hivyo rais Bashir amesisitiza kwamba waziri huyo hakuhusika katika visa vya uhalifu wa kivita.

Afisa mmoja wa mahakama ya mjini The Hague amesisitiza umuhimu wa kuwashtaki washukiwa wa uhalifu katika mzozo huo wa Darfur

´Ni muhimu sana sio tu kwa mzozo wa Darfur bali duniani kote hususan barani Afrika kwamba anayekiuka haki za binadamu atakabiliwa na mashtaka wakati huo au baadaye.´

Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, amesema hali ya Darfur ni ya kuvunja moyo, lakini la muhimu ni kwamba mchakato wa kisiasa bado unaendelea kuutanzua mzozo huo.