1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kiir aitisha mjadala wa kitaifa wa amani

15 Desemba 2016

Rais wa Sudani Kusini Salva Kiir ameitisha mjadala wa kitaifa utakaojadili namna ya kumaliza machafuko na mustakabali mzima wa nchi hiyo inayokabiliwa pia na kitisho cha machafuko ya kikabila

https://p.dw.com/p/2UItq
Südsudan Präsident Salva Kiir
Picha: picture-alliance/dpa/P. Dhil

Mjadala huo unaitishwa na Rais Kiir, baada ya hatua mbalimbali zilizofikiwa zilizolenga kusimamisha mapigano, ambazo hazijaweza kuleta matumaini ya kurejea kwa amani nchini Sudani Kusini wakati ambapo nchi hiyo inatimiza miaka mitatu ya mapigano ya wenyewe kwa wenyewe. 

Kwenye hotuba yake mbele ya bunge, Kiir anayegombania madaraka na aliyekuwa makamu wake Rieck Machar amesema mdahalo wa kufatuta maridhiano  utaimarisha hatua za kuleta amani nchini humo. Amesema watu mashuhuri watakaozungumzia wasuluhishi wataongoza mjadala huo utakaohusisha watu wote wa Sudani Kusini, ingawa hakutaja wajumbe wa jopo hilo.

Nia mahusisi ya mjadala huu ni kuiepusha nchi na mpasuko na kusaka enzi mpya ya amani, utulivu na ustawi. Majeshi ya Kiir yanalaumiwa kwa kusababisha mauaji ya kimbari, ubakaji, na unyanyasaji wa kingono na kuwalazimisha watoto kujiunga na jeshi. Aidha, vikosi vyake vinashutumiwa kwa mauaji ya kikabila yaliyotokea hivi karibuni, Kusini mwa mji wa Yei, hali inayoashiria kuibuka kwa mauaji wa kimbari.

Hata hivyo, Kiir mwenyewe kwenye hotuba hiyo amesema, atakabiliana vilivyo na wale wanaojihusisha na kusambaza chuki za kikabila, huku akikemea wale wanaopinga uwepo wa Jumuiya za kimataifa nchini humo na juhudi wanazofanya za kuleta amani.
 
Vita vya Sudan Kusini vimeendelea kusambaa na kugubika maeneo mengi zaidi nchini humo, amesema mchambuzi Alan Boswell, ambaye anatabiri kuongezeka kwa mashambulizi makubwa zaidi hasa kwenye majira ya kiangazi. Amesema, pande zinazokinzana zimekuwa zikiwapa mafunzo askari wapya, wakati ambapo wanadipolasia wakifanya jitihada za kuzuia machafuko hayo.   

Südsudan Kindersoldaten
Ripoti ya Umoja wa Mataifa inasema raia wengi hususan watoto wameandikishwa kujiunga na jeshi kwa hiyari ama kwa kulazimishwaPicha: picture alliance/AA/UNICEF/S. Rich

 

Umoja wa Mataifa: Watoto wanakabiliwa na uonevu na unyanyasaji mkubwa.

Ripoti ya Umoja wa Mataifa imesema kiasi ya watoto 1,300 nchini Sudani Kusini wamepewa mafunzo ya kijeshi mwaka huu, na kufanya idadi kufikia zaidi ya watoto 17,000 tangu kuzuka kwa mapigano kati ya Rais Salva Kiir na aliyekuwa Makamu wake Rieck Machar. 

Ripoti hiyo iliyotolewa na shirika na Umoja wa Mataifa linaloshughulikia watoto, UNICEF imesema tangu mwezi Novemba shirika hilo limeandikisha kiasi ya watoto 50 waliotekwa na kupewa mafunzo ya kijeshi katika eneo la Kaskazini mwa jimbo la Upper Nile pekee. Waasi na jeshi la serikali pamoja na wahirika wao wameshutumiwa kwa kutoa mafunzo hayo.

Ripoti hiyo imesema watoto hao pia wanakabiliwa na unyanyasaji. Tangu mwaka 2013 UNICEF na washirika wake waligundua visa 2,342 vya watoto kuuwawa, 1,130 kunyanyaswa kingono na visa 303 vya mashambulizi. Pamoja na watoto wanawake nao wanatajwa kuathirika kwa mashambulizi na unyanyasaji wa kingono amesema Yasmin Sooka, mwenyekiti wa tume ya haki za binaadamu nchini Sudani Kusini.

Machafuko nchini Sudani Kusini yalianza mwezi Decemba mwaka 2013, wakati Rais Salva Kiir alipomtuhumu aliyekuwa makamu wake Rieck Machar kuaandaa mapinduzi. Makubaliano ya amani yaliyosainiwa miaka miwili na nusu baadae yaliibua matumaini ya kumaliza machafuko hayo yaliyosababisha makumi kwa maelfu ya raia kuuwawa na wengine takriban milioni 3 kuyakimbia makazi yao.

Hata hivyo, makubaliano hayo yalidumu kwa miezi miwili tu na kuzuka tena kwa machafuko hatua iliyosababisha Machar kutoroka na sasa akiishi uhamishoni nchini Afrika Kusini.

Mwandishi: Lilian Mtono.
Mhariri: Saumu Yusuf.