1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaJamhuri ya Kongo

Kikosi cha EAC chaanza kuondoka kutoka Kongo

Tatu Karema
3 Desemba 2023

Kikosi cha Jumuiya ya Afrika Mashariki kilichotumwa Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, kimeanza kuondoka leo asubuhi nchini humo baada ya serikali ya nchi hiyo kusema hakitekelezi majukumu yake ipasavyo

https://p.dw.com/p/4Zio8
Wanajeshi wa kikosi cha Jumuiya ya Afrika Mashariki wakiwa mjini Bunagana katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo mnamo Aprili 19, 2023
Wanajeshi wa kikosi cha Jumuiya ya Afrika Mashariki nchini KongoPicha: Alain Uaykani/Xinhua/picture alliance

Kulingana na msemaji wa kikosi hicho nchini Kongo, kundi la kwanza la takriban wanajeshi 100 wa Kenya kutoka kikosi hicho ambacho pia kinajumuisha wanajeshi wa Uganda, Burundi na Sudan Kusini, liliondoka kutoka uwanja wa ndege wa Goma kuelekea Nairobi.

Shirika la habari la AFP limeripoti kuona ndege iliyobeba wanajeshi hao ikiruka muda mfupi baada ya saa kumi na moja alfajiri.

Soma pia: Congo yataka vikosi vya Afrika Mashariki viondoke DRC

Lakini mapigano bado yanaendelea kati ya kundi la M23 na jeshi la Kongo ambalo linaungwa mkono na wanamgambo wanaojiita "wazalendo".

Jumuiya hiyo ya kikanda ilipeleka wanajeshi wake kwa mara ya kwanza katika eneo lililokumbwa na ghasia nchini Kongo mnamo mwezi Novemba mwaka jana baada ya kuibuka upya kwa kundi la waasi la M23.