1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kim Jong Un aagiza kuundwa kwa makombora zaidi

John Juma
23 Agosti 2017

Kiongozi wa Korea Kaskazini aamuru kuundwa kwa makombora madhubuti na vichwa vya nyuklia nchini mwake. Wakati huohuo, Rais Trump asema huenda uhusiano wao na Pyongyang ukaimarika.

https://p.dw.com/p/2igWq
Nordkorea Militärparade Symbolbild
Picha: Getty Images/AFP/E. Jones

Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un ameamuru taasisi ya jeshi inayounda silaha nchini mwake kuunda maroketi zaidi yenye nguvu. Shirika la habari la serikali ya nchi hiyo KCNA imetangaza hayo leo. Haya yanajiri wakati kukiwa na mzozo kati ya Marekani  na Korea Kaskazini kuhusu mipango ya makombora na nyuklia. Hata hivyo zipo dalili zinazoonesha kuwa mzozo huo unatulia.

Ripoti hiyo ambayo imetangazwa na shirika la habari linalomilikiwa na serikali ya nchi hiyo KCNA, haikuwa na vitisho dhidi ya Marekani kama ilivyokuwa katika wiki kadhaa zilizopita.

Runinga hiyo ya KCNA imeonesha picha za Kim Jong Un akizuru taasisi ya kemikali ya kijeshi, ambapo alielezewa hatua za kuunda makombora ya masafa marefu ya nyuklia pamoja na maroketi yenye injini za nguvu zaidi.

Msomaji habari wa kituo hicho amesoma kuwa "Kim Jong Un ameagiza kuundwa kwa zana zaidi. Ameiagiza taasisi hiyo kuunda maroketi zaidi yenye injini madhubuti na vichwa vya nyuklia, pamoja na kuimarisha injini kutumia nyenzo za kemikali ya kaboni."

Kim Jong Un na Donald Trump
Kim Jong Un na Donald TrumpPicha: picture alliance/AP Photo

Trump: Kim Jong Un ameanza kuheshimu Marekani

Kauli ya Kim Jong Un inajiri muda mfupi baada ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Rex Tillerson kuonekana akitoa kauli ya amani na kuonekana akipongeza kile alichosema kuwa ni Korea Kaskazini kujizuia katika siku za hivi karibuni. Rais wa Marekani Donald Trump ameelezea matumaini ya uwezekano wa uhusiano wa nchi hizo mbili kuimarika.

Akizungumza kuhusu mzozo wao na Korea Kaskazini, alipouhutubia mkutano wa hadhara jimboni Arizona, Trump amesema: "Ninaheshimu kwamba Kim Jong Un ameanza kutuheshimu. Ninaheshimu hilo sana. Na labda au jambo la maana litatokea, lakini hawatakuambia hilo kuwa labda jambo chanya linaweza kupatikana."

Kim Jong Un akikagua jaribio la kurushw akwa kombora la masafa marefu
Kim Jong Un akikagua jaribio la kurushwa kwa kombora la masafa marefuPicha: Getty Images/AFP/KCNA

China yaonya kuhusu vikwazo vipya

Wakati huo huo, China imeonya dhidi ya vikwazo vipya vya Marekani vinavyolenga makampuni ya China na Urusi yanayohusishwa na Korea Kaskazini, ikisema havitasaidia ushirikiano wao kutatua mzozo kuhusu nyuklia.

Mnamo siku ya Jumanne, Wizara ya fedha ya Marekani iliyalaumu makampuni yaliyolengwa kwenye vikwazo hivyo, kuwa yanaunga mkono mipango ya nyuklia ya Korea Kaskazini na kujaribu kukwepa kutekeleza vikwazo vya Marekani.

Vikwazo vipya vimejiri wakati Rais Trump akiongeza shinikizo kwa Beijing kuwajibika zaidi kuishawishi Korea Kaskazini ambayo ni mshirika wake mkuu kuachana na malengo yake ya nyuklia.

Tangu mwaka uliopita, Korea Kaskazini imefanya majaribio mawili ya kinyuklia na mengine kadhaa ya kufyatua makombora hali ambayo imezua taharuki katika rasi ya Korea.

Mwandishi: John Juma/RTRE/AFPE

Mhariri:Josephat Charo.