1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kiongozi wa Iran awasili New York kulihutubia baraza kuu la umoja mataifa

Mohammed AbdulRahman24 Septemba 2007

Kutoa mihadhara miwili leo juu ya msimamo wa nchi yake kuhusu masuala mbali mbali yenye mabishano na jumuiya ya kimataifa huku ziara yake hiyo ikikabiliwa na upinzani.

https://p.dw.com/p/CB12
Rais Ahmadinejad wakati akiondoka Teheran Jumapili.
Rais Ahmadinejad wakati akiondoka Teheran Jumapili.Picha: AP

Rais Mahmoud Ahmadinejad ambaye ametoa wito wa kuangamizwa dola ya Israel ma kuhoji juu ya mauaji ya halaiki ya wayahudi, atakihutubia kikao cha baraza kuu la umoja wa mataifa kesho. Rais Ahmadinejad alisema kabla ya kuondoka Teheran jana kwamba ziara hiyo itampa nafasi kuweaza kukutana na wanasiasa wa kujitegemea kutoka taifa hilo kubwa na hasimu wa Iran na pia kuipa nchi yake nafasi ya kujieleza mbele ya jukwaa la kimataifa.

Alinukuliwa na shirika la habari FARS akisema kwamba “ Baraza kuu la umoja wa mataifa ni nafasi nzurio ya kuwasilisha suluhisho la watu wa Iran, kuyatatua matatizo ya dunia.” Akiongeza “ Tunapaswa kuzitumia nafasi kama hizi kufafanua misimamo ya watu wa Iran kwa kuwa wao Wamarekani wanahamu kubwa ya kuisikia."

Ziara hii ya Rais wa Iran imekabiliwa na upinzani nchini Marekani, ambayo imeishutumu Iran kwa kujaribu kuunda bomu la nuklea na kumzingatia Kiongozi wa Iran kuwa mshirika wa wanaharakati wanaowashambulia wanajeshi wa Marekani nchini Iraq.

Akizungumza katika mahojiano na televisheni ya CBS yaliofanywa tangu wiki iliopita mjini Teharan, Rais Ahmadinejad alionekana kutozipa uzito hoja hizo za kutaka kuwa na silaha ya nuklea akisema hawaihitaji na kuuliza tunahitaji bomu la nini ? Alisema ni kosa kufikiria Iran na Marekani zinataka kuingia vitani na kuuliza tena , Kwa nini tuingia vitani ?

Ziara ya Ahamadinejad inafanyika katika wakati ambao uhusiano wa nchi yake na Marekani uko katika kiwango cha chini kabisa huko nchi hizo mbili zikiwa hazina uhusiano wa kibalozi tangu 1979 baada ya mapinduzi ya Kiislamu nchini iran.

Hata kabla ya kuwasili Newyork kwa azma hiyo ya kulihutubia baraza kuu la umoja wa mataifa, tayari wanasiasa mjini humo na jumuiya za Wayahudi, wameendesha upinzani mkubwa kupinga ziara hiyo na kukiataka chuo kikuu cha Columbia kutomualika kiongozi huyo wa Iran kutoa mhadhara chuoni humo. Jana kiasi ya waandamanaji 100 walikusanyika nje ya chuo hicho wakiwa na mabango yenye maandishi ya kumpiga Ahmadinejad.

Lakini akiutetea uamuzi wao, Rais wa chuo hicho kikuu Lee Bollinger alisema chuo kikuu cha Columbia ni jamii iliojizatiti katika kutoa elimu na kujifunza na kuheshimu fikra zinazopingana. Alisema atautumia uwanja huo kumapa chanaga moto Ahmadinejad kuhusiana na matamshi yake juu ya mauaji ya halaiki dhidi ya Wayahudi, wito wake wa kuangamizwa Israel na suala la Iran kutaka kuwa na silaha ya nuklea na upinzani wa jumuiya ya kimataifa.

Waandamanaji zaidi wanaatarajiwa kukusanyika katika Chuo kikuu cha Columbia leo na wairan wanaoishi uhamishoni wakiwa wapinzani wa utawala wa Iran wanapanga kuandamana nje ya makao makuu ya umoja wa mataifa kesho wakati Rais Ahmadinejad atakapofika kulihutubia baraza kuu .

Marekani ikiwa mwenyeji wa umoja wa mataifa inalazimika chini ya mkataba wa kimataifa unaohusiana na itifaki ya kibalozi kuwaruhusu waakilishi wa mataifa yote wanachama kulitembelea eneo lolote umbali wa kilomita 40 kutoka makao makuu ya umoja wa mataifa