1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kisa cha mahabusi wa Uengereza

Oummilkheir5 Aprili 2007

Kuachiwa huru wanamaji wa kingereza ndio mada iliyohanikiza magazetini nchini Ujerumani hii leo

https://p.dw.com/p/CHTJ

Tuanze na alifu lakini ambapo gazeti la LANDESZEITUNG la mjini LÜNEBURG linammulika rais wa Iran na kuandika:

“Licha ya madaha yake anapotoa aya za Qoraan,Ahmadinedjad ni mpiga hesabu mwerevu kabisa.Angeuacha mvutano uzidi makali,asingejipatia faida anazojivunia hivi sasa:faida nono inayotokana na biashara ya mafuta pamoja pia na kusifiwa na majirani zake.Picha za maafisa wakoloni wa zamani,wasiopendwa na walioingiwa na hofu,wanaokiri kwamba wamevunja mipaka,pamoja na mwanajeshi wa kike aliyelazimika kufunga hijab zinapewa uzito mkubwa na waarabu wa madhehebu ya sunni.Wafarsi ambao ni wa madhehebu ya shiya wanazidi kujitokeza kama jamii yenye usemi mkubwa katika eneo la Ghuba.”

Mod:

Gazeti la THÜRINGER ALLGEMEINE la mjini ERFURT linahisi Ahmadinedjad alikua amebanwa.Gazeti linaendelea kuandika:

“Kufika hadi ya kuutaja uamuzi wa kuwaachia huru kua ni jaza kwa Uengereza,inaonyesha wazi kabisa kwa jinsi gani serikali ya mjini Teheran ilikua imebanwa.Hakuna shaka yoyote,kwa kuwateka nyara wanamaji hao wa Uengereza,vichwa mchungu miongoni mwa walinzi wa mapinduzi ya kiislam walitaka kuingilia kati katika siasa ya nje ya Iran.Baada ya kuzidishwa makali vikwazo vya Umoja wa mataifa dhidi ya Iran kutokana na kuendelea nchi hiyo kurutubisha maadini ya Uranium,vichwa mchungu hao hawakutaka kuwaachia viongozi waregeze kamba,badala yake walidhamiria kuzidisha makali ya mzozo huo.Rais Ahmadinedjad hakuweza kuridhia.Badala yake ameamua kuwatunukia nishani maafisa wanaohusika na wakati huo huo kuwatuliza nyoyo waengereza.”

Mod:

Gazeti la FRANKFURTER ALLGEMEINER ZEITUNG linaandika:

„Bila ya kuingilia kati mkuu wa mapinduzi Ali Chamenei hakuna lolote ambalo lingeweza kutendeka.Kadhia hii ilipangwa tangu mwanzto kua chanzo cha kupimana nguvu nchini Iran.Walinzi wa mapinduzi,anakotokea pia Mahmut Ahmadinedjad wangeendelea kuwashikilia wanamaji hao.Lakini kuna wengineo miongoni mwa viongozi wa Iran ambao hawakupendezewa na yaliyotokea kinyume na rais ambae moyo haumdundi hata kama jamhuri ya kiislam ingezidi kutengwa.Wenye kufuata msimamo wa wastani wamefanya kila la kufanya kuepusha nchi yao isizidi kutengwa kimataifa.“

Mod:

Gazeti la STUTTGARTER ZEITUNG linaandika kuhusu mradi unaobishwa wa kinuklea wa Iran:

„Viongozi wa Iran hawakujaribu kulitumia suala la mahabusi kama chambo katika mvutano kuhusu madi wa kinuklea.Hakuna shaka yoyote walitaka kuuonyesha ulimwengu mzima,Iran si dola la kigaidi kama nchi za magharibi zinavyohoji.Pasiwe na yeyote atakaetarajia kwamba Teheran itakua pia maridhia katika mvutano wake kuhusu mradi wa kinuklea na kutekeleza masharti ya nchi za magharibi.Panapohusika na suala la haki yake ya kurutubisha maadini ya Uranium,Iran kattu haitotetereka.Na hapo viongozi wa Iran,wanazungumza kwa sauti moja,licha ya misimamo yao inayotofautiana.