1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kizaazaa cha Bundesliga kuendelea wikendi hii

Admin.WagnerD11 Machi 2016

Bayern Munich hawajashinda katika mechi zake mbili za mwisho na mshambulaiji Thomas Mueller anasema hawastahili tena kupoteza pointi nyingine zaidi za Bundesliga wakati wakipambana leo na Werder Bremen

https://p.dw.com/p/1IBwM
Bayern München Thomas Müller
Picha: picture-alliance/dpa/L. Perenyi

Uongozi wa Bayern kileleni mwa msimamo wa ligi umepunguzwa hadi pointi tano baada ya kuduwazwa na Mainz na kutoka sare ya bila kufungana na nambari mbili Borussia Dortmund. Huku ikisalia michuano tisa msimu kukamilika, Bayern chini ya Kocha Pep Guardiola inataka kuwa klabu ya kwanza kushinda mataji manne mfululizo ya Bundesliga.

Dortmund wana mchuano mgumu ugenini dhidi ya Mainz kesho Jumapili wakati ambapo kocha Thomas Tuchel anarejea katika klabu yake ya zamani. Nambari tano Mainz waliimarisha matumaini y BVB katika kinyanng'anyiro cha taji kwa kuwabwaga Bayern mbili moja hivi karibuni na vijana hao wa kocha Martin Schmidt pia waliwabwaga Schalke na Bayer Leverkusen katika wiki za karibuni.

Mshambuliaji wa BVB Pierre-Emerick Aubameyang anarejea katika vita vyake na Lewandowski kuwa mfungaji wa magoli mengi katika ligi ambapo mshambuliaji huyo wa Gabon ana mabao 22, moja nyuma ya nyota huyo wa Bayern raia wa Poland

Wolfsburg watapambana na nambari mbili kutoka nyuma Hoffenheim wakati wachezaji wake Julian Draxler na Andre Schuerrle wakiwa katika hali bora kabisa. Washika mkia Hannover watawaalika Cologne leo huku timu zote zikikabiliwa na kitisho cha kushushwa ngazi. Katika mechi nyingine za leo, Borussia Moenchengladbach v Eintracht Frankfurt, Ingolstadt v VfB Stuttgart, Darmstadt v Augsburg. Kesho Jumapili Bayer Leverkusen v Hamburg

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA
Mhariri: Daniel Gakuba