1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Klopp aurefusha mkataba wake hadi 2018

30 Oktoba 2013

Kocha Jürgen Klopp ametia saini ya kuurefusha mkataba wake katika klabu ya Borussia Dortmund kwa miaka miwili zaidi hadi mwaka wa 2018. Klabu ya Dortmund inastahili kujivunia sana kazi anayowafanyia

https://p.dw.com/p/1A9FY
Jürgen Klopp ni mpenzi wa mashabiki wengi, pamoja na wachezaji wake
Jürgen Klopp ni mpenzi wa mashabiki wengi, pamoja na wachezaji wakePicha: picture-alliance/dpa

Klopp ambaye ni mmoja wa makocha wanaomezewa mate sana barani Ulaya, alijiunga na Dortmund mwaka wa 2008, na kuwaongoza kunyakua taji la Bundesliga mwaka wa 2011 pamoja na ligi ya nyumbani na kombe la shirikisho katika mwaka wa 2012 kabla ya kushindwa na mahasimu wao wa Ujerumani Bayern Munich katika fainali ya Champions League msimu huu.

Huku akianzisha enzi ya kabumbu safi la kasi na kuvutia, ambalo limewavutia mashabiki wengi kote ulimwenguni, kuwasili kwa Klopp kulifungua ukurasa mpya kwa mabingwa hao wa Champions League mwaka wa 1997 ambao nusra wafilisike kabisa takribani miaka kumi iliyopita.

Klopp amewaambia waandishi wa habari baada ya kusaini mkataba huo kuwa “hakuna anayestahili kupiga simu hadi mwaka wa 2018”. Amesema wanahisi kuwepo imani kubwa na matumaini katika klabu hiyo na hiyo ni dalili nzuri.

Amesema ni heshima kuwa baadhi ya vilabu vikuu ulimwenguni vinaona kuwa BVB inafanya kazi nzuri lakini yeye siyo sehemu ya wale wanaohisi kuwa kuna lishe nzuri zaidi kwingineko. Mikataba ya wafanyakazi wenzake katika klabu hiyo pia imerefushwa katika juhudi za kuendeleza mafanikio ambayo wamepata katika miaka ya karibuni.

Mwandishi: Bruce Amani/Reuters

Mhariri: Josephat Charo