1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kocha wa Ujerumani aanza maandalizi ya kombe la Euro 2012

Sekione Kitojo28 Desemba 2011

Kocha wa Ujerumani Joachim Löw aanza kujiandaa kwa fainali za kombe la mataifa ya Ulaya kukiwa kumesalia miezi sita, wakati premier league nyasi zaanza kuwaka moto leo

https://p.dw.com/p/13ZT4
Kocha wa timu ya taifa ya Ujerumani Joachim Löw akiangalia mchezo wakati timu ya Ujerumani ikiwa uwanjani .
Kocha wa timu ya taifa ya Ujerumani Joachim Löw akiangalia mchezo wakati timu ya Ujerumani ikiwa uwanjani.Picha: picture-alliance/dpa

Tuanzie  hapa  Ujerumani : wakati  ikisalia  miezi  sita  kabla ya  michuano  ya  fainali  za  kuwania  ubingwa  wa  mataifa ya  Ulaya, Euro  2012   michuano  itakayofanyika  huko Poland  na  Ukraine,  kocha  wa  Ujerumani  Jogi Löw anaendelea  na  maandalizi   ya  fainali  hizo, licha  ya kuwa  kwa  sasa  ligi  ya  Ujerumani  imo  mapumzikoni. Lakini  muda  huu  si  mrefu  sana , na  pamoja  na  hayo timu  ya  Ijurumani  itakuwa  na  mchezo  mmoja  tu  wa majaribio  dhidi  ya  Ufaransa  kabla  ya  kuingia  katika kinyang'anyiro  hicho. Ni  eneo  gani  hasa  Jogi  Löw analolenga  kulishughulikia  kwa  sasa  katika  maandalizi ya  timu  yake :  kocha  wa  Ujerumani  Joachim Löw amesema .

"Tunaangalia  kwa  kweli  wachezaji  wetu. Wakati  tuna mchezo  mmoja  tu  wa  kimataifa  wa  kujipima  nguvu, ni kawaida  kwamba  inabidi   uangalie  wachezaji  wako katika  vilabu, hususan  katika  mapambano  yao.  Jicho pia  tunatupia  kwa  wapinzani  wetu , kwa  hiyo utakapoanza  mwezi  wa  Januari  tutaongeza  kasi  ya kuzichunguza  Ureno, Uholanzi  na  Denmark, na tutajishughulisha  zaidi  pia  na  wachezaji  mmoja  mmoja, ambapo  tutasema , tufanye  nini  ili  kuwafanya  wachezaji mmoja  mmoja  kuwa  bora  zaidi, tutatawapa  nini  cha zaidi  wachezaji  wetu  katika  kusakata  soka,  na  kati  gani muhimu  tunayopaswa  kuifanya   katika  wiki  za maandalizi, ili  tuweze   katika   kinyang'anyoro  hiki kufanya  vizuri, na  kuweka  kiwango  cha  soka  yetu  juu" .

Kocha  wa  Ujerumani  Joachim Löw  akijibu  swali kuhusu  ni  maandalizi  gani  anayoyafanya  kabla  ya kuingia  viwanjani  mwezi  wa  Juni  katika  kinyang'anyiro cha  kombe  la  mataifa  ya  Ulaya , euro  2012.

Wakati  huo  huo  mchezaji  nyota  chipukizi  wa  Ujerumani na  Borussia  Dortmund  Mario  Goetze anashauku  kubwa na  michuano  hiyo   ya  fainali  za  kombe  la  mataifa   ya Ulaya  nchini  Poland  na  Ukraine. Goetze , ambaye amecheza  mchezo  wake  wa  kwanza  wa   kimataifa  na timu  ya  taifa  ya  Ujerumani  dhidi  ya  Sweden  Novemba mwaka  huu ,  amesema   jana   kuwa  anashauku  kubwa ya  kuwamo  katika  kikosi  cha  kocha  Joachim Löw  na kushiriki  katika  mashindano  hayo.

Mchezaji nyota chikupikizi wa Ujerumani Mario Goetze akipachika bao katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Brazil mwaka huu.
Mchezaji nyota chipukizi wa Ujerumani Mario Goetze akipachika bao katika mchezo wa kirafiki dhidi ya Brazil mwaka huu.Picha: picture-alliance/dpa

Hayo  yatakuwa  mashindano  yake  ya  kwanza  makubwa. Ujerumani  itakwaana  na  Ureno, Uholanzi  na  Denmark katika  kundi  B katika  mashindano  hayo.

Na  bado  tukiwa  katika  soka  la  Ujerumani  Schalke  04 imepata  huduma  ya  mshambuliaji  kutoka  Nigeria Chinedu Obasi  kwa  mkopo  kutoka  Hoffenheim   pia  ya Ujerumani , hadi  utakapomalizika  msimu  huu ,  lakini kwa  masharti  kuwa  inawezekana  kurefusha  mkataba huo , iwapo  Schalke  watapendezwa  na  huduma  ya Obasi.

Mshambuliaji  huyo  anamkataba  na  Hoffenheim  hadi mwaka  2014, tangu  mwaka  2007. Mchezaji  huyo  wa Nigeria  ameichezea  Hoffenheim  mara  65  na  kufunga mabao  13  lakini  kwa  hivi  sasa  amepoteza  nafasi  yake katika  kikosi  cha  kwanza  cha  Hoffenheim.

Katika  Premier league  sasa, Meneja  wa  zamani  wa Chelsea  Jose  Mourinho  ana  lengo  la  kurejea  katika Premier League  atakapomaliza  muda  wake  katika  klabu ya  Real  Madrid, amesema  hayo  leo  Jumatatu. Nina furaha  sana  kuwapo  Madrid , Mourinho  amesema  katika kipindi  cha  radio 4  cha BBC  cha  "Today". Sikutaka kupoteza  fursa  ya  kufanyakazi  hapa  lakini  shauku yangu  ni  Uingereza  na  hatua  yangu  ijayo  itakuwa kurejea  huko, iwapo  itawezekana, na  nikiwa  huko nitakaa  kwa  muda  mrefu, amesema  Mourinho, ambaye mkataba  wake  wa  miaka  minne  na  Real  unamalizika mwishoni  mwa  msimu  wa  2013-14. Kipindi  chake  cha miaka  mitatu  na  Chelsea  kilimalizika mwaka  2007  na alikwenda  Italia akaiongoza  Inter Milan  hadi  ubingwa  wa champions League, ikiwa  ni  ubingwa  wake  wa  pili  wa kombe  hilo kufuatia  ule  wa  mwaka  2004  akiwa  na  FC Porto.

Nae meneja  wa  Arsenal  Arsene  Wenger  anakiri  kuwa ratiba  ya  michezo  ya  Premier  League  katika  wakati huu  wa  siku  kuu  ya  Chrismas  ambapo  timu  hiyo inaumana  na  Wolves, Qeens Park Rangers  na  Fulham inaweza   kutoa  picha  ya  msimu  huu   kwa  timu  hiyo. Arsenal  ambayo  inapambana  na  Wolves  kesho Jumanne , iko  points  mbili  tu  mbele  ya  Liverpool ambayo  iko  nafasi  ya   sita , lakini  iko  points  moja  tu nyuma  ya  timu  iliyoko  nafasi  ya  nne Chelsea.

Kocha wa Arsenal London Arsene Wenger
Kocha wa Arsenal London , Arsene WengerPicha: picture-alliance/dpa

Wenger  amesema  kuwa  anafahamu  kuwa   timu  yake ina  nafasi  ya  kujisogeza  juu  zaidi  ya  msimamo  wa  ligi . Na  akaongeza, Ni  wajibu  wetu  kufanyakazi  hiyo.

Wakati  huo  huo , Wenger  anaamini  bahati  yake  ya kupata  mchezaji  wa  nafasi  ya  ulinzi  wa  kushoto inawasi  wasi , lakini  hajatoa  ombi  lolote  la  kupata  mtu atakayeshikilia  nafasi  hiyo  kwa  muda. Wenger  alibaki bila  ya  kuwa  na  mchezaji  halisi  ya  nafasi  hiyo  ya ulinzi  wa  kushoto  baada  ya  Kieran Gibbs  kufanyiwa upasuaji  katika  paja   Alhamis  wiki  iliyopita. Gibbs anatarajiwa   kuwa  nje  ya  uwanja  kwa  mwezi  mmoja na  anajiunga  na  mchezaji  mwenzake  wa  nafasi  hiyo Sandro  Santos  ambaye  naye  ameumia.

Cesc  Fabregas  wa  Barcelona  amesema   jana   kuwa ana  matumaini  ya  kumaliza  muda  wake  wa  kucheza soka   na  Barcelona, lakini  iwapo  ataondoa  katika  timu hiyo  kigogo  cha  soka   la  Uhispania  atarejea  tu  Arsenal London  na  sio  kwingineko. Mbali  ya  Arsenal  na Barcelona  sioni  timu  nyingine  ambayo  naweza kuichezea , amsema  mchezaji  huyo  wa  kiungo  mwenye umri  wa  miaka  24. Wakati  nikiwa  na  nafasi  ya kuangalia  mchezo  nakwenda  Arsenal , kukutana  na mafariki  na  mashabiki , na  huwezi  kujua  hapo  baadaye naweza  kurejea  Arsenal.

Nina  matumaini  kuwa  nitabakia  hapa  kwa  muda  mrefu , na  hata  kustaafu  , lakini  nani  anajua , katika  maisha huwezi  kusema  haiwezekani.  Na  kama  kuna  sehemu nyingine  naweza  kwenda , ni  Arsenal  , hiyo  ni  hakika amesema  Frabregas.

Naye  mchezaji  wa  kiungo  wa  Barcelona  Seydou Keita ameteuliwa  jana  Jumapili  kuwa  mchezaji  bora  wa mwaka  2011  nchini  Mali. Keita  ambaye  atakuwa miongoni  mwa  wachezaji  wanaounda  kikosi  cha  timu ya  taifa  ya  Mali  katika  kinyang'anyiro  cha  kombe  la mataifa  ya  Afrika  mwezi  ujao, ameisaidia  Barcelona kunyakua  taji  la  ubingwa  wa  Ulaya  Champions  League , ligi  ya  Uhispania, La  Liga, na  kombe  la  dunia   la vilabu  hivi  karibuni  nchini  Qatar.

Mchezaji  wa  Tottenham  Hot Spurs  Emmanuel Adebayor anaamini  kuwa  msukumo  wa  timu  ya  Manchester  City kuwania  kunyakua  ubingwa  wa  ligi  msimu  huu unaweza  kuingia  matatani  kutokana  na  mashindano  ya kombe  la  mataifa  a  Afrika  mwakani. City  watakosa huduma  ya  ndugu  wawili  muhimu  katika  kikosi  hicho yaya  Toure  na Kolo  Toure  ambao  watajiunga  na  kikosi cha  Cote D'Ivoire  kwa  ajili  ya  michuano   hiyo  inayoanza Januari 21  hadi  February 12, wakati  Spurs  haitaathirika kwa  kuwa  Togo  ambako  Adebayor  anatoka  imepigwa marufuku  kushiriki  mashindano  hayo.

Adebayor  amesema  kuwa  City  ni  timu  nzuri, yenye  ari kubwa  na  kwa  wakati  huu  inacheza  soka  safi  kabisa , lakini  wakipata  majeruhi  wachache , nafikiri  itakuwa vigumu  sana  kwao.

Sir Alex Ferguson  amekataa  wazo  la  kutokuwepo   na changamoto  kubwa   kutoka  mjini  London  kileleni  mwa msimamo  wa  ligi  ya  Uingereza  Premier League mwakani  licha  ya  timu  mbili  za  mjini  Manchester kutamalaki . Uwezo  mkubwa  ulioonyeshwa  na Manchester  United  na   viongozi  wa  ligi  hiyo  kwa  sasa Manchester City  umesababisha  wadadisi  wengi  wa mambo  ya  soka  kuamini  kuwa  bingwa  atatoka  katika mji  wa  Manchester. Hata  hivyo , licha  ya  kuwa Tottenham  iliyo  katika   nafasi  ya  tatu  kwa  sasa  iko nyuma  kwa  points  saba  nyuma  ya  Manchester  United , lakini  kikosi  cha  kocha  Harry  Redknapp  kina  mchezo mmoja  zaidi na  historia  imemfunza  kocha  wa  siku nyingi  wa  Manchester  United  kuwa  changamoto  dhidi ya  nia  yao  ya  kulinyakua  tena  taji  hilo  inaweza  kutoka katika  vyanzo  mbali  mbali  katika  mwaka  mpya.

Na  huko  nchini  Hispania , mshambuliaji  wa  Barcelona David Villa  ametoka  hospitalini  siku  tano  baada  ya kufanyiwa  operesheni  katika  mguu  wake  uliovunjika wakati  wa   michuano  ya  kombe  la  dunia  la  vilabu nchini  Qatar.

Mchezaji wa Barcelona na Hispania ambaye amevunjika mguu.
Mchezaji wa Barcelona na Hispania David Villa ambaye amevunjika mguu.Picha: AP/dapd

Mshambuliaji  huyo  wa  kimataifa   wa  Hispania, Villa bingwa  wa  dunia  na  kombe  la  champions League, anatarajiwa  kubakia  nje  ya  uwanja  hadi  miezi  mitano, na  kwamba   ushiriki  wake  katika  kombe  la  mataifa  ya Ulaya euro  2012  uko   mashakani.

Watu  wenye  ulemavu  watapatiwa  tiketi  za  bure 32,000 kuingia  katika  michezo  ya  kombe  la  dunia  mwaka 2014  nchini  Brazil. Hayo  yamesemwa  na   chama  cha mpira  wa  miguu  nchini  Brazil  ambacho  kimetoa  bure tiketi  hizo, ambapo  zitagaiwa  kwa  mpango  wa  tikiti  500 kwa  kila  mchezo. Gharama  itakuwa  kiasi  cha  euro milioni  10. Mchezaji  wa  zamani  wa  timu  ya  taifa  ya Brazil Ronaldo  amesema.

"Mara  nyingi  wenye  ulemavu  huwa  hawafikiriwi  katika mashindano  kama  haya . Tunataka  kubadilisha  hali hiyo. Hatuwasahau  watu  wenye  ulemavu."

Mshambuliaji  wa  zamani  wa  Brazil  ambaye  alikuwa bingwa  wa  dunia  katika  kikosi  cha  Brazil  mwaka  1994, Romario  ambaye  ni   mbunge  katika  bunge  la  Brazil   tangu mwaka  2010   ameamua  kuchangia   sehemu  ya  tiketi hizo  za  bure  kwa  walemavu.

Mwandishi : Sekione  Kitojo / ZR / afpe /dpae

Mhariri: Othman Miraj