1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kombe la klabu bingwa Afrika

21 Julai 2008

Al Ahli yailaza Zamalek katika kombe la Afrika la klabu bingwa 2:1.

https://p.dw.com/p/EgMc

Kombe la klabu bingwa -kanda ya Afrika mashariki na kati limeingia hatua ya robo-finali.Al Ahly, mabingwa mara 5 wa kombe la klabu bingwa barani Afrika watamba mbele ya mabingwa mara 5 wengine Zamalek katika kinyan'ganyiro cha kombe la klabu bingwa barani Afrika.Dynamo ya Zimbabwe imeipiku ASEC Abidjan ya Corte d' Iviore.

Mwenyekiti wa Chelsea, Peter Kenyon amekanusha Chelsea kujitolea kutoa kitita kikubwa kabisa kilicho-rekodi kumvutia kaka wa Brazil ili kujiunga nao kutoka AC Milan-aliungama hatahivyo, kuwa bado wanamtapia mno Robinho kutoka Real Madrid.

Na Rafael van der Vaart-stadi wa Holland atabakia alao msimu huu na klabu yake ya Hamburg katika Bundesliga.

Tuanze moja kwa moja na changamoto ya jana ya kukata na shoka kati ya mabingwa 2 waliotwaa kila mmoja kombe la klabu bingwa barani Afrika mara 5 na mahasimu wakubwa nyumbani Cairo: Al Ahly na Zamalke.

Ahmed Hassan,stadi mpya wa Al Ahly, aliufumania jana mlango wa Zamalek kwa bao maridadi la mkwaju wa "free-kick" na kumaliza mchezo kwa ushindi wa mabao 2:1.

Hassan akiichezea mara ya kwanza Al Ahly baada ya kuiachamkono Anderlecht ya Ubelgiji,alilifumania lango hilo la Zamalek mnamo dakika ya 67 ya mchezo na hivyo kuhakikisha ushindi kwa Al Ahli.Katika kinyan'ganyiro cha kumuania yeye,Al Ahly iliipiku Zamalek na kumuajiri Hassan mapema mwaka huu.

Al Ahly iliufumania kwanza mlango wa Zamalek mnamo dakika ya 28 ya mchezo pale muangola Gilberto alipompokonya dimba Abdallah na kumtupia mwenzake pia kutoka Angola-Flavio kuunasa wavu wa Zamalek.

Mnamo dakika ya 63 ya mchezo,Zamalke iliambia Al Ahly "kutangulia si kufika."

Gamal Hamza alisawsazisha.

"Niliwaonya wachezaji wangu kabla ya mechi hii kuwa mshindi itaibuka ile timu itakayofanya makosa machace kuliko mwenziwe."-alisema kocha wa Zamalek mjerumani Reiner hollamnn ambae miaka 10 nyuma alikuwa wa al Ahli.

Hassan alieiongoza Misri kutwaa kombe la Afrika la mataifa mapema mwaka huu nchini Ghana,alisema amesisimkwa mno na bao lake la kwanza kwa Al Ahly. Mwenzake Emad Moteab alibebwa kitikiti mabegani na wenzake uwanjani mwishoni mwa mechi hii,kwani anawaachamkono kujiunga na Bristol City ya Uingereza.

Junior Agogo kutoka Ghana, alieichezea Zamalek kwa mara ya kwanza tangu kujiunga nayo kutoka klabu yake ya uingereza ya Nottingham Forest hakufua dafu na akatolewa nje ya uwanja dakika 15 za mwisho.

Ushindi wa Al Ahly,umewapeperusha kileleni mwa kundi A pamoja na Dynamo ya Zimbabwe .Dynamo iliitimua jana ASEC Abidjan ya Ivory Coast mjini Harare .Timu nyengine 2 zilishinda jumamosi-Conton sport ya kamerun na Al Hilal ya Sudan.

Kutoka kombe la klabu bingwa -champions league, tugeukie kombe la klabu bingwa kanda ya Afrika mashariki na kati mjini Dar-es-salaam,Tanzania. Kinyan'ganyiro hiki kimeingia hatua ya robo-finali huku mabingwa watetezi APR ya Ruanda, wamerudi kutamba baada ya kutelezwa mbele ya Miembeni ya Zanzibar . Sasa wana miadi kesho na simba ya Tanzania.

Bundesliga-Ligi ya Ujerumani, bado haikuanza msimu wake mpya lakini, klabu za daraja ya kwanza na ya pili zimo kujinoa kambini na hasa mabingwa Bayern Munich.

Stadi wa Holland,Rafael van der Vaart anaichezea klabu ya Hambgurg katika Bundesliga alitamani ,kuhamia Real Madrid msimu huu.

Kulikuwapo fununu kwamba,Real ya Spain ikitaka kumuajiri ,lakini sasa yaonesha kwamba van der Vaart atabidi kubakia katika klabu yake ya hamburg msimu mpya.

"nimeshajitolewsa kucheza msimu mwengine katika klabu ya Hamburg." -alisema van der vaart.

Majira haya ya kiangazi yalitoa fursa ya mwisho kwa Hamburg kuweza kumuuza stadi wao huyo kwa kitita kikubwa cha fedha.Hamburg ingetumia kura yake ya turufu kuzima kiu cha van der vaart kujiunga na klabu yoyote maarufu barani Ulaya kama vile Real Madrid.

Van der Vaart alijiunga na hamburg 2005 na mkataba wake unadumu hadi 2010.

Katika Premier League-Ligi ya Uingereza,mwenyekiti wa Chelsea Peter Kenyon alikanusha leo kuwa chelsea imekuwa tayari kutoa kitita kikubwa kilicho-rekodi kumuajiri stadi wa Brazil Kaka kutoka AC milan ya Itali.

Aliungama lakini,Chelsea ingali bado ikimtapia mbrazil mwengine Robinho kujiunga nao.Robinho anaichezea Real Madrid.

Chelsea karibuni imemfungisha mkataba stadi wa timu ya taifa ya Ureno wa asili ya Brazil-Deco ili kuimarisha kikosi chake.

Stadi wa kiungo alie staafu kuichezea timu ya taifa ya Ufaransa Cluade Makelele, anajiunga na paris st.Germain kutoka chelsea ya Uingereza.Makelele alipangwa kutembezwa leo mbele ya waandishi habari mjini Paris.

OLIMPIK BEIJING 2008:

Michezo ya olimpik ya Beijing ikikaribia na wanariadha wa Afrika ma hasa Kenya na Ethiopia wakijinoa kupepea bendera ya bara hilo huko Beijing, hebu tulitupe leo macho bara la Asia na matumaini yao huko Beijing:

Kundi la nchi za kusini-mashariki mwa Asia-ASEAN huenda likawakilisha wa na wanariadha kutoka nchi 10 zenye wakaazi jumla ya nusu-bilioni.

Kinyume na bara la Afrika, kundi la ASEAN lilimudu kunyakua medali 12 tu huko Athens,Ugiriki, 2004.Hakuna pia matumaini ya kwamba mara hii michezo hii ikirudi Asia, baada ile ya seoul, 1988, zitaondoka hapo August 24 siku ya mwisho ya michezo na medali zaidi ya hizo darzeni 1.

Katika medali 12 zilizonyakuliwa na wanariadha wa ASEAN-8 zilikwenda Thailand-tatu katiya hizo zikiwa za dhahabu.Indonesia ikanyakua medali 4 kati ya hizo 1 ya dhahabu. Singapore,Malaysia,Vietnam,Brunei,Laos,Cambodia, Philipines na Myanmar zilitoka mikono mitupu bila ya hata medali moja.

Kwa mara nyengine tena,Thailand ina matumaini ya kutamba na kurudi na medali zaidi kuliko wenzake. Thailand inatamba sana katika ringi ya mabondia na kunyanyua vyuma vya wezani mzito kwa wanawake.Kama Thailand, wasichana wa Indonesia nao wanatia fora katika kubeba vyuma vya wezani mzito.

Ku ndi la ASEAN, nchi za kusini -mashariki mwa asia, zinatawala mchezo wa badminton duniani na ni ,katika mchezo huu ndipo malaysia inatumai kuongezea medali zake ilizonyakua hadi sasa: 1 ya fedha na 2 za shaba.

Singapore muda mfupi uliopita imekuwa ikijiandaa kuwa Mecca ya michezo katika eneo la ASEAN.na ndio itakayokuwa mwenyeji wa michezo ya kwanza ya olimpik kwa vijana 2010 na ina kiu kuona wanariadha wake wanatamba katika daraja ya kimataifa.