1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Korea kaskazini yaendelea na ukaidi yafyatua kombora jingine

Sekione Kitojo
29 Aprili 2017

Korea kaskazini imefanya jaribio la kombora leo Jumamosi(29.04.2017)Korea ya kusini na jeshi la Marekani zimesema,ikikaidi onyo la Marekani na,China, zilizojaribu kwa miaka kadhaa kudhibiti mpango wa silaha wa nchi hiyo.

https://p.dw.com/p/2c6yB
Nordkorea provoziert mit weiterem Raketentest
Makombora ya Korea kaskazini yakifyatuliwaPicha: Getty Images/AFP/Str.

Jaribio  hilo  lililofanywa  katika  eneo kaskazini mwa  mji  mkuu  wa Korea  kaskazini , Pyongyang, linaonekana  kuwa  limeshindwa, maafisa  wa  Marekani  na  Korea  kusini wamesema, katika  kile ambacho  ni jaribio  la  nne  mfululizo  la  Korea  kaskazini kushindwa  tangu  mwezi  Machi.

Jaribio  hilo linakuja  wakati  waziri  wa  mambo  ya  kigeni  wa  Marekani Rex Tillerson amelionya baraza  la  Usalama  la  Umoja  wa  Mataifa  kwamba  kushindwa  kuudhibiti mpango  wa  kinyuklia  na  makombora  wa  Korea  kaskazini  kunaweza  kusababisha "matokeo  mabaya".

UN Sicherheitsrat - US-Außenminister Rex Tillerson zu Nordkorea
Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Rex TillersonPicha: Reuters/L. Jackson

Maafisa  wa  Marekani , wakizungumza  kwa  masharti ya  kutotajwa majina, wamesema kombora  hilo huenda  ni  la  masafa  ya  kati  linalofahamika  kama KN-17 na  linaonekana kuwa liliripuka  na  kuvunjika  katika  muda  wa  dakika  chache  tangu  pale lilipofyatuliwa.

Korea kusini  imesema nchi  hiyo  ya  kaskazini  inacheza  na  moto  na  kuionya  kwamba itakabiliwa  na  vikwazo  vikali  zaidi  ya  Umoja  wa  Mataifa.

Ukiukaji wa maazimio ya Umoja wa Mataifa

Jeshi  la  Korea  kusini  limesema  kwamba  kombora  hilo , lililofyatuliwa  kutoka  katika jimbo  la  Pukchang  katika  mwelekeo wa  kaskazini  mashariki, lilifikia  umbali  hewani  wa kilometa 71  kabla  ya  kuvunjika vunjika  dakika  chache  wakati  likiruka. Limesema kurushwa  kwa  kombora  hilo  ni  ukiukaji  wa  wazi  wa  maazimio  ya  Umoja  wa  Mataifa na kuionya  Korea  kaskazini kutochukua  hatua  bila  kufikiria.

US Navy Destroyer USS Mason - DDG 87
Moja kati ya meli za kivita za Marekani USS Mason - DDG 87Picha: picture-alliance/dpa/A. Delgado

Utawala  wa  rais  wa Marekani  Donald Trump  unaweza  kuchukua  hatua  dhidi  ya  jaribio hilo  la  kombora  la  Korea  kaskazini  kwa  kuharakisha  mipango  yake kwa  ajili  ya vikwazo  vipya  vya  Marekani  dhidi  ya  Pyongyang, ikiwa  ni  pamoja  na  uwezekano  wa hatua  dhidi  ya maeneo  mahususi  ya  Korea kaskazini  na  China, afisa  wa  Marekani ameliambia  shirika  la  habari  la  Reuters jana.

Wakati Korea  kaskazini  inachukua  hatua kwa  kukaidi  mbinyo  kutoka  Marekani  na mshirika  wake  mkubwa  China, Marekani  inaweza  kufanya  luteka mpya  ya  jeshi  la  majini na  kuweka  meli  zaidi  za  kijeshi  na  ndege  katika  eneo  hilo  kwa  nia  ya  kuonesha uwezo  wa  nguvu  zake , afisa  huyo  amesema , kwa  masharti  ya  kutotajwa  jina.

US Flugzeugträger USS Carl Vinson
Meli iliyobeba ndege za kivita za Marekani USS carl VinsonPicha: Reuters/U.S. Navy photo/M. Castellano

Vikwazo vipya

Afisa  huyo  amesema  vikwazo vyovyote  vipya  vinaweza  kuwekwa  katika  siku  chache zijazo na  vinaweza  kulenga  idadi  kadhaa  ya  maeneo  ambayo  tayari  yametathminiwa  na serikali  ya  Marekani  kwa  ajili  ya  hatua  kama  hizo, wakati  utawala  huo  wa  Marekani unaendelea  kutayarisha  mpango  mkubwa  zaidi  wa  vikwazo.

Maeneo  lengwa  ya vikwazo hivyo , afisa  huyo  amesema , yanaweza  kuwa  taasisi  za  kifedha  na  makampuni  muhimu ya  Korea kaskazini  pamoja  na  China, hatua  ambayo  huenda  ikaikasirisha  China.

USA Präsident Donald Trump bei der NRA - National Rifle Association
Rais wa Marekani Donald TrumpPicha: Reuters/J. Ernst

Wakati  rais  Trump  amemsifu  rais  wa  China Xi Jinping kwa  kuashiria ongezeko  la ushirikiano kuhusiana  na  suala  la  Korea kaskazini , afisa  huyo  amesema  Beijing  bado "inahitajika  kuchora  aina  fulani  ya  msitari mchangani" na  Pyongyang kuhusiana  na mpango  wake  wa  kinyuklia.

Hatua  za kijeshi  chini  ya  hatua  zinazofanyiwa  tathmini  ni  pamoja  na  kuonesha  uwezo wa  nguvu  za  Marekani  katika  eneo  hilo  zenye  lengo la  kuizuwia  Korea  kaskazini  na kuihakikishia  Korea  kusini  mshirika  mkubwa  wa  Marekani  kuhusu  usalama  wake, ameeleza  afisa  huyo  wa  Marekani.

Mwandishi: Sekione  Kitojo / rtre

Mhariri: Idd Ssessanga