1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Leverkusen bado kileleni mwa Bundesliga

15 Februari 2010

Bayern Münich inaifuata nyuma

https://p.dw.com/p/M1ve
Gomez , Roben na Mueller washangiria bao la Munich.Picha: AP

Katika Bundesliga, Bayer Leverkusen iko bado pointi sawa na Bayern Munich kileleni mwa Bundesliga -

Katika robo-finali ya Kombe la FA nchini Uingereza,mabingwa wa Kombe hilo FC Chelsea,wana miadi ama na Manchester City au Stoke City .

Kinyan'ganyiro cha Kombe la klabu bingwa barani Afrika, kimeanza kwa timu za Tanzania kushindwa kufua dafu.

Na michezo ya olimpik ya majira ya baridi, inaendelea huko Vancouver,Kanada huku wanariadha wa Marekani wakiongoza orodha ya medali huku Kanada na Ujerumani zikiwa ni miongoni mwa mataifa yalionyakua medali.

Bundesliga:

Nahodha wa Bayern Munich ,Mark van Bommel na mdachi mwenzake Arjen Robben, kila mmoja alitia bao kukamilisha ushindi wa Bayern Munich wa mabao 3-1 hapo Jumamosi dhidi ya Borussia Dortmund na sasa wako bao 1 tu nyuma ya viongozi wa ligi Bayer leverkusen.Timu zote mbili zina pointi sawa 48,lakini Leverkusen, ina magoli 30 kwa 29 ya Munich.Leverkusen ilitokwa na jasho kabla kuwatimua mabingwa VBFL Wolfsburg kwa mabao 2:1.

Schalke, iliipiga kumbo FC Cologne kwa mabao 2:0 na kubakia nafasi ya 3 ya ngazi ya ligi nyuma ya Munich wakati Hamburg ikitamba kwa mara ya kwanza nyumbani na jogoo lake kutoka Holland, Ruud van Niestelrooy, ilikomea Stuttgart mabao 3:1 .Van Niestelrooy, aliitwa dakika ya 75 ya mchezo kuteremka uwanjani na dakika hiyo hiyo alilifumania lango la Stuttgart kwa bao lake la kwanza kabisa katika Bundesliga .Dakika 2 baadae, van Niestelrooy,utamua ukamkolea na akatia tena bao lake la pili.

Kocha wa Bayer Leverkusen,viongozi wa Ligi Jupp Hynckes, aliueleza hivi mpambano wake na mabingwa Wilfsburg:

"Leo tumecheza na mabingwa na tulipata taabu sana kutamba.Kipndi cha pili timu yetu ilianza kutia fora,lakini tulichoshindwa ni kwamba , baada ya kutia bao ,hatukuweza kukamilisha sawa sawa mashambulio yetu."Alsema kocha wa viongozi wa Bundesliga Hynckes.

Nae kocha wa mahasimu wake Bayern Munich ,mdachi van Gaal alieleza:

"Nimefurahi mno kuwa, tumeshinda kwavile, Dortmund ilicheza uzuri sana na kwa nguvu sana.Kwahivyo, nimeridhika mno."

Nae jogoo la Holland na Real Madrid, van Niestelrooy lililoazimwa kwa Hamburg,lilianza kuwika alipotia mabao 2 katika ushindi wa mabao 3:1 dhidi ya Stuttgart.Mwishoe, van Niestelrooy akasema:

"Nina hisi uzuri sana kujiunga na Hamburg na Bundesliga na nina matamanio mengi.Nitajaribu kutia mabao zaidi, ingawa hii haitawezekana kila mechi."

FC Cologne ilipata pigo lake la kwanza tangu kupita mapambano 8 ilipolazwa na Schalke kwa mabao 2:0.Baadae stadi wa FC Cologne, Lukas Podolski alisema:

"Hasa wakati huu wa sherehe za kanivali ambapo wakaazi wa Cologne wanasherehekea kama wenda-wazimu na hapa uwanjani kuna mashabiki 6000 wa Cologne , na inatia uchungu sana kushindwa."

PREMIER LEAGUE:

Premier League, ilipumzika mwishoni mwa wiki kuacha nafasi kwa Kombe la taifa la FA: Mabingwa wa Kombe hilo Chelsea, watacheza ama na Manchester City au Stoke City katika changamoto ya robo-finali mwezi ujao.Hii inatokana na kura iliopigwa jana.Ikiwa Manchster City itailaza Stoke City katika mpambano wa marudioano Februari 24,basi Chelsea, itaweka miadi na Manchester city.Timu hizi mbili pia zina miadi hapo Feb.27 kwa mpambano wa Premier League.

Mwandishi:Ramadhan Ali /RTRE/DPAE

Uhariri:Abdul-Rahman