1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

LONDON : Kifo cha Diana ni ajali sio mauaji

10 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CCkZ

Repoti iliokuwa iksubiriwa kwa muda mrefu juu ya kifo cha Princess Diana katika ajali ya gari mjini Paris itathibitisha uchunguzi wa Ufaransa kwamba ilikuwa ni ajali na kufuta nadharia kwamba kifo hicho ilikuwa ni njama za majasusi wa Uingereza.

Kwa mujibu wa habari zilizovuja leo hii juu ya repoti hiyo ya Lord John Stevens kamishna wa polisi wa zamani wa jiji kuu la London imehitimisha kwamba Diana alikufa katika ajali ya gari baada ya dereva wake kupoteza udhibiti wa usukani wakati akiwa amelewa.

Wakiwakimbia wapiga picha mapaparazi Diana aliyekuwa na umri wa miaka 36,mpenzi wake Dodi Fayed mwenye umri wa miaka 42 na dereva wao Henri Paul aliekuwa na umri wa miaka 41 walikufa katika ajali hiyo ya gari kwenye sehemu ya barabara inayopita barabara nyengine juu yake ya Paris alfajiri ya tarehe 31 mwezi wa Augusti mwaka 1997.

Repoti hiyo itatumika kufuta mawazo ya nadharia za njama zinazodai kwamba sampuli za damu ya Paul zilibadilishwa ili kuonyesha kuwa alikuwa amelewa.

Mmiliki wa duka kubwa la Harrods Mohammed al Fayed kwa muda mrefu amekuwa akisisitiza kwamba mwanawe na Diana waliuliwa na njama ya utawala wa Uingereza kwa lengo la kumzuwiya mke wa zamani wa Prince Charles mrithi wa Ufalme wa Uingereza kufunga ndoa na Muislamu.

Repoti hiyo pia inatazamiwa kutupilia mbali nadharia nyengine kuhusu njama kwamba Diana alikuwa mjamzito na kwamba alikuwa amepanga kufunga ndoa na Dodi.