1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Maafa ya Chernobyl yakumbukwa

26 Aprili 2011

Maafa makubwa yameisibu Tschernobyl; miaka 25 baadae serikali zilitaraji maafa hayo yangekuwa yameshamalizika na kusahauliwa. Kwa wananchi lakini maafa hayo bado mpaka leo yanamaanisha uchungu na huzuni.

https://p.dw.com/p/1140D
Mishumaa kuwakumbuka wahanga wa TschernobylPicha: AP

Ilikua siku ya Jumamosi, April 26, miaka 25 iliyopita, kinu cha nne cha kinyuklea kiliripuka huko Tschernobyl, katika eneo la Jamhuri ya zamani ya Usovieti, Ukraine. Vladimir Anatolevich Gudov, wakati ule alikuwa kijana na kutumika kama mwanajeshi wa akiba katika jeshi la Usovieti. Hapajapita muda aliamrishwa kwenda katika eneo hilo la maafa.

"Katika kipindi cha miezi saba, siku 206, usiku na mchana, tutakawa tunafanya kazi kukifunika kwa seruji kinu hicho nambari nne. Wakati ule, hiyo ilikuwa kazi ngumu kupita kiasi." Anasema Vladimir.

Vladimir Gudov alikuwa miongoni mwa wafanyakazi laki nane waliokuwa wakijulikana kama "Wamiminaji",waliokua na jukumu la kuzuwia kwa kila hali mionzi ya hatari ya kinyuklea isivuje toka mtambo huo ulioripuka. Walitakiwa wazuwie mionzi ya kinyuklea isiendelee kuenea katika anga ya Usovieti, Ulaya na kutapakaa kote ulimwenguni. Mionzi mtu hawezi kuiona, hainuki na wala mtu hawezi kuonja ina ladha ya aina gani. Na pia watu hawakuarifiwa vya kutosha kuhusu hatari ya mionzi hiyo.

Ukraine Tschernobyl Reaktor 4
Kinu cha 4 cha kinuklea cha TschernobylPicha: DW

Svetlana Kabanzova, mwalimu wa kijerumani huko Kostjukovitschi, Byelorussia, anaelezea kuhusu siku ya mwanzo ya maafa hayo makubwa. Alikuwa njiani na gari yake. Anasema:

"Ninakumbuka jinsi tulivyokwama katika njia ya mchanga inayopita mashambani. Wakulima walikuwa wakilima mashambani mwao, licha ya vumbi la mionzi ya kinyuklea. Bila ya shaka, watoto wadogo pia walikuwa wakicheza nje kwa sababu hali ya hewa ilikuwa nzuri kupita kiasi."

Palipita muda hadi maafisa wa serikali walipoamuru watu wahamishwe kutoka maeneo yaliyoadhirika zaidi na mionzi hiyo ya kinyuklea.

Denkmal am Reaktor in Tschernobyl
Kumbusho la waliofanyakazi katika kinu cha kinuklea cha TschernobylPicha: DW/K.Percy

Kwa wengi, uamuzi huo haukuwasaidia kitu-walifariki au kushikwa na magonjwa ambayo mpaka leo yanazidi kuongezeka. Mionzi ya kinuklea iliyowapiga wakati ule sio tuu imewasababishia maradhi ya saratani ya kila aina,hata maradhi ya moyo na kiharusi yamewadhuru watoto na vijana, na wengine kushikwa na maradhi ya kiakili, viungo vya mwili kutokuwa ipasavyo au hata kuzeeka kabla ya wakati.

Valentina Smolnikova ni daktari,amekuwa akiwashughulikia wengi kati ya wahanga wa mionzi ya kinyuklea ya Tschernobyl katika mkoa wa Gomel, Byelorussia. Anasema Tschernobyl na Fukushima ni hatari kupita vita.l

Mwandishi:Mast-Kirschning,Ulrike/Hamidou Oummilkheir

Mhariri:Miraji Othman