1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Magazetini Ujerumani

15 Julai 2010

Mada kuu katika magazeti ya Ujerumani leo Alkhamisi ni kuchaguliwa kwa waziri mkuu wa jimbo la North Rhine Westphalia lenye wakaazi wengi kabisa nchini Ujerumani.

https://p.dw.com/p/OJi2
Die neue Ministerpräsidentin von Nordrhein-Westfalen, Hannelore Kraft (SPD), wird am Mittwoch (14.07.2010) im nordrhein-westfälischen Landtag in Düsseldorf vereidigt. Gut neun Wochen nach der NRW- Landtagswahl wurde die 49-Jährige mit den Stimmen von SPD und Grünen im zweiten Wahlgang zur Chefin einer Minderheitsregierung gewählt. Foto: Julian Stratenschulte dpa/lnw
Waziri Mkuu mpya wa jimbo la Ujerumani la North Rhine Westphalia,Hannelore Kraft.Picha: picture alliance / dpa

Kiwango cha chini kabisa cha mishahara ya wafanyakazi wanaowatazama wazee, ni miongoni mwa masuala mengine yaliyoshughulikiwa na wahariri wa magazeti ya Ujerumani leo . Basi tutaanza na gazeti la NÜRNBERGER ZEITUNG linalosema:

"Haitokuwa rahisi hivyo kwa serikali kuendesha kazi zake katika jimbo lenye wakaazi wengi kabisa nchini Ujerumani.Hata miongoni mwa vyama vya SPD na Kijani vilivyounda serikali hiyo ya muungano kuna shaka iwapo mfumo wa serikali hiyo una uwezo wa kudumu. Bila shaka Waziri Mkuu na mawaziri wake wanataka kuhakikisha kuwa watabakia madarakani kwa awamu yote. Wakati huo huo, upande wa upinzani wa vyama vya CDU na FDP katika serikali ya jimbo la North Rhine Westphalia wanapaswa kucheza karata zao vizuri.Kwani kuna hatari ya kupoteza zaidi umaarufu wao ikiwa watakwamisha kazi za serikali mpya. Kwa hivyo vyama hivyo havina budi kujipanga upya kisiasa katika bunge la düsseldorf na hata katika serikali kuu mjini Berlin. Ama sivyo watapata pigo jingine iwapo kutafanywa uchaguzi mpya katika jimbo la NRW."

Kwa maoni ya gazeti la FINANCIAL TIMES la Ujerumani, Waziri Mkuu Hannelore Kraft alieshika wadhifa huo baada ya kuchaguliwa hiyo jana katika bunge la Düssedorf, anataka kuthibitisha kuwa anaweza kuiongoza serikali katika wakati ulio mgumu, hata chini ya mfumo wa vyama vitano bungeni. Gazeti hilo linaongezea:

"Jaribio hilo halitofanikiwa.Kwani Waziri Mkuu Kraft atagundua haraka kuwa haitokuwa rahisi hivyo kupitisha miradi muhimu. Ufunguo wa kupata uwingi bungeni upo mikononi mwa chama cha Die Linke. Lakini baadhi ya wafuasi wa chama hicho wanangángania sera kali za mrengo wa kushoto kwa hivyo si chama kinachoweza kutegemewa. Na vyama vya CDU na FDP vitajaribu kupinga miradi ya serikali ya Bibi Kraft, hata kama itaambatana na sera zake kisiasa."

Kwa upande mwingine gazeti la FLENSBURGER TAGEBLATT linasema:

"Serikali ya mseto ya vyama vya SPD na Kijani katika jimbo la North Rhine Westphalia, itaipa msukumo mpya serikali ya muungano wa vyama vya CDU/CSU na FDP mjini Berlin kuwa na umoja kuliko jitahada zote za hapo awali. Kwani ghafula, muungano huo umegundua kuwa SPD na Kijani si vyama vya kupuuzwa tena. Waziri Mkuu Kraft amedhihirisha kuwa ana kipaji cha kuhimili matatizo."

Tunamalizia kwa mada nyingine - yaani kiwango cha chini cha mshahara wa watunza wazee.Gazeti la BERLINER ZEITUNG linasema:

"Kwa kuweka kiwango cha chini cha mishahara ya wafanyakazi wanaowatazama wazee, hakutosababisha nafasi za ajira kupotea. Ukweli ni kwamba jamii inayozidi kuwa na wazee inawategemea wafanyakazi hao. Lakini hatua ya kuweka kiwango cha chini cha mshahara haitosaidia kuwavutia vijana kusomea kazi hiyo. Hatua iliyochukuliwa imeondosha tu hali mbaya ya malipo iliyokuwepo, kwani hata katika siku zijazo, wafanyakazi hao hawatolipwa mishahara wanayostahili kupata."

Mwandishi:P.Martin/DPA

Mhariri: M.Abdul-Rahman